SUAMEDIA

Serikali yaahidi kusambaza na kuendeleza mfumo wa uhifadhi na usimamizi shirikishi wa misitu ya asili nchini

 Calvin Gwabara

Morogoro.

Serikali imeahidi kusambaza na kuendeleza mfumo wa uhifadhi na usimamizi shirikishi wa misitu ya asili kwenye wilaya zote nchi nzima ili kulinda misitu hiyo na kuwezesha vijiji kunufaika na uwepo wa mistu kwenye maeneo yao baada ya mbinu hiyo kuonesha mafanikio makubwa kwenye Vijiji vya awamu ya kwanza na ya pili ya mradi.


Afisa Misitu Mkuu Idara ya Uratibu wa Maliasili na Mazingira kutoka Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Bw. Sanford Kway akizungumza na waandishi wa habari

Ahadi hiyo imetolewa na Afisa Misitu Mkuu Idara ya Uratibu wa Maliasili na Mazingira kutoka Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Bw. Sanford Kway wakati akiongea na waandishi wa habari nje ya mkutano wa uwasilishwaji wa matokeo ya tafiti saba zilizofanywa na wadau mbalimbali katika maeneo ya yanayotekeleza Mradi wa CoFOREST ambao unatekelezwa na Shirika la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG) na Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa Misitu Tanzania (MJUMITA).

“Kweli tunatambua kuwa mradi unaisha na mafanikio haya kama serikali hatutamani yaishie hapa ndio maana kwenye awamu ya tatu ya mradi tumekubaliana kwamba watekeleze kwenye Kijiji kimoja kimoja kwenye kila wilaya mpya za mradi ili iwe sehemu ya wao kuwajengea uwezo wataalamu wa halmashauri kuelewa vyema mfumo huu ili nao wasambaze kwenye vijiji vingine na kweli tunaona kuna uendelevu” Alisema Bw. Kway.

Amesema progamu hiyo ina manufaa makubwa kwa Serikali kwa sababu kuwezesha waananchi kusimamia ile misitu yao na wao kupitia motisha wanayoipata kuna sababisha wao kuwa walinzi wazuri maana wanaona kuna manufaa wanayapata hivyo hawawezi kuacha iharibiwe bali watailinda na kuivuna kwa uendelevu.


                           Magunia ya Mkaa yaliyotayarishwa kwenda sokoni

Afisa Misitu Mkuu huyo Idara ya Uratibu wa Maliasili na Mazingira kutoka TAMISEMI amekiri kuwa katika wilaya tatu za awamu ya kwanza za Mkoa wa Morogoro wananchi wameweza kutumia kile wanachokipata katika kufanya shughuli nyingi za kijamii kama vile kujenga miundombinu ya shule, zahanati, ofisini za vijiji na Bima za Afya ambayo pengine Serikali isingeweza kuyafanya kwa haraka hivyo.

“ Tunafahamu kuwa vijiji kupitia mapatoa yao wanarejesha asilimia 10 ya mapato kwenye halmashauri ambazo baadae kiasi hutakiwa kurudishwa kwenye vijiji au kutumiwa na maafisa wa halmashauri kufanya shughuli za ugani kwenye vijiji lakini hii imekuwa changamoto kwenye vijiji vingi vya mradi huu na Serikali imeliona na kuliwekea mkakati mzuri ambao ukikamilika utasaidia halmashauri kuzirejesha kwa wakati “ Alifafanua Bw Kway.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Utafiti wa Matumizi ya Misitu ya Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI) Dkt. Chelestino Balama amesema kuwa yale yote yanayofanywa na mradi huo wa CoFOREST yanapata ushauri kutoka TAFORI maana wao ni sehemu ya wajumbe wa kamati ya ushauri katika utekelezaji wake.


Kaimu Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Utafiti wa Matumizi ya Misitu ya Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI) Dkt. Chelestino Balama akitolea ufafanuzi baadhi ya mambo juu ya mradi huo

Amesema mawasilisho hayo ya tafiti saba yanatokana na ushauri wao kuwa wakati mradi ukiendelea lazima kufanyike tafiti mbalimbali ambazo zitasaidia kupatikana takwimu sahihi na ushahidi wa kisayansi ambao utawezesha maamuzi yoyote yatakayofanywa na Serikali.

“Mradi huu kama utasimamiwa vizuri unaweza kuwa suluhisho la changamoto za uharibifu wa misitu ya asili iliyo kwenye ardhi za vijiji maana tumetembelea kwenye vijiji vyote vinavyotekeleza mradi na tumeona kwa macho yetu namna walivyoweka mfumo mzuri wa uvunaji ambao kweli ni endelevu lakini kubwa tunaomba kuwepo kwa mahusiano mazuri na misimamo kwa viongozi wa vijiji katika utekeelzaji ili kuwepo na uendelevu” amesema Dkt. Balama.


            Magogo ya miti yakitayarishwa kwa ajili ya kutengeneza mkaa

Mradi huu unaendeshwa TFCG na MJUMITA kupitia Mradi wa Usimamizi Shirikishi wa Misitu ya Jamiii (USMJ) unatekelezwa chini ya Mradi wa kuleta Mageuzi katika Sekta ya Mkaa Tanzania (TTCS) Mradi wa kuhifadhi Misitu kwa Kuwezesha Biashara Endelevu ya Misitu (CoFOREST) kwa ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Uswis (SDC).

Post a Comment

0 Comments