SUAMEDIA

Chuo cha Kilimo na Mifugo Kaole kilichopo Bagamoyo kimeipongeza SUA kwa kazi nzuri za kuinua vijana

 

Gladness Mphuru

SUA

Mkuu wa Chuo cha Kilimo na Mifugo Kaole kilichopo Bagamoyo Bw. Sinani Simba, amesema watashirikiana na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kwa sababu mbali na kubobea katika utoaji bora wa elimu pia inachangia katika kupunguza ukosefu wa ajira kwa vijana kupitia kilimo.

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Prof. Raphael Chibunda katikati akiwa na Mkuu wa Chuo cha Kilimo na Mifugo Kaole Bw. Sinani Simba wa tatu kutoka kushoto na ujumbe kutoka Kaole na SUA wakiwa katika mazungumzo

Bw. Simba ametoa kauli hiyo leo tarehe 21, Aprili 2022 katika Kampasi ya Edward Moringe Sokoine mkoani Morogoro, wakati wa ziara yao ya kukitembelea chuo cha SUA akiwa ameambatana na viongozi mbalimbali wa SUA ambapo amepata mapokezi kutoka kwa mwenyeji wake Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Prof. Raphael Chibunda.

Mkuu huyo wa Chuo cha Kaole, amesema kuwa SUA mbali na kutoa elimu kwa wanafunzi pia imetoa fursa kwa wananchi hususan vijana, kupitia kituo atamizi kwa ajili ya vijana wajasiriamali kinachoitwa PASS AIC SUA, ambao wanapatiwa elimu, wanapewa maeneo ya kulima ndani ya chuo pamoja na mikopo nafuu.

“atamizi hiyo inaonesha dhamira chanya ambayo inaonesha kwamba SUA mmepania katika kupunguza ukosefu wa ajira kwa vijana, lakini pia mnawaonesha wanafunzi kufanya kwa vitendo wakitoka hapo wanaenda kuwa wakulima wazuri na kuwanufaisha wengine” amesema Simba


Mkuu wa Chuo cha Kilimo na Mifugo Kaole Bw. Sinani Simba wa tano kutoka kulia akisikiliza maelezo katika Hospitali ya Rufaa ya Wanyama nchini iliyopo SUA

Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo hicho Maximilian Sarakikya, amesema ushirikiano baina yao ya SUA utawasaidia kuwaleta wanafunzi wao kuja kujifunza kwa vitendo, kuleta sampuli zao hususani za udongo kuja kuchunguzwa, sambamba na kuomba ushirikiano na wataalamu wa SUA kuwaongezea maarifa hususani kwenye tafiti.

“tumejifunza mengi sana kutoka kwa wenzetu SUA, wenzetu wametupita ngazi kubwa zaidi lakini tumejifunza mengi ambayo yatatusaidia baadae na katika ushirikiano wetu kuna mambo ambayo wenzetu watatushika mkono hususani Maktaba kwa Machapisho ya Kilimo na pia tumejionea jinsi wanafunzi wanavyotakiwa kusoma kwa vitendo” amesema Sarakikya

Akizungumza kwa niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha SUA Dkt. Alex Matofali ameushukuru ugeni huo kwa kuzuru Kampasi hiyo, na kuwaahidi kuyafanyia kazi yote waliyoyapendekeza hasa kupokea wanafunzi ili wajifunze kwa vitendo.

Post a Comment

0 Comments