SUAMEDIA

Zaidi ya Asilimia 60 ya Udongo Morogoro, Rukwa, Mbeya umepoteza virutubisho

 

Na.Vedasto George.

Utafiti uliofanywa katika mikoa ya Morogoro, Rukwa, Mbeya  na Iringa umebaini kuwa asilimia 60 hadi 70 ya udongo katika mikoa hiyo umepoteza virutubisho vyake na kusababisha wakulima wa mazao ya mahindi, alizeti, viazi na mpunga  kutopata mazao yenye ubora na  tija na kusababisha familia nyingi kuendelea kuwa masikini.

 

Picha Mtandaoni

Hayo yamebainishwa na  Mtafiti wa Udongo kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania -TARI  Uyole na Kiongozi wa Mradi wa Uboreshaji wa Kilimo Bora kwa Wakulima FREDRICK MLOWE ambapo amesema  utafiti huo umefanyika katika vijiji 400 vya mikoa hiyo na kubaini  virutubisho vya msingi katika udongo vimepotea kutokana na matumizi  mabaya ya ardhi.

“Udongo wa maeneo yote tuliyopita umechoka, ukosefu wa kirutubisho cha zinki peke yake  katika udongo kwenye kilimo cha mpunga unaweza ukapelekea mkulima kukosa mavuno kwa asilimia 30 mpaka 35 lakini uwepo wa upungufu wa kirutubisho cha Sulpha kwenye udongo mkulima anaweza kukosa mavuno kwa asilimia 70, kwa hiyo ardhi yetu katika mikoa hii imechoka sana”, amesema Mtafiti huyo.

  Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya Kilimo TARI  Uyole Dkt.TULOLE  LUGENDO amesema licha ya udongo kutokuwa na virutubisho vya kutosha lakini  bado mazao mengine yanaweza kulimwa katika mikoa hiyo.

“Kitu kingine ambacho tumekigundua ni kwamba kuna uwezekano wa kuanzisha mazao mapya  ambayo yalikuwa hayajazoeleka, mazao kama michikichi, kokoa na makadamia yanaweza kulimwa na wakulima wakapata faidia kubwa”, amesema Dkt. Lugendo.

 Mhandisi JUMA MDEKE Kaimu Mkurugenzi Idara ya Mipango na Matumizi Bora ya Ardhi kutoka Wizara ya Kilimo amesema Wizara itaendelea kushirikiana na wadau wa kilimo nchini ili kukifanya kilimo kiweze kuwanufaisha wakulima na taifa kwa ujumla.

“Sisi watu wa sera tunasema ili upate tija ni lazima kufahamu Afya ya udongo ya maeneo husika basi sisi kama wizara tutahakikisha matokeo haya yaliyopatikana kwenye utafiti huu  yanatumika  kwa sababu dhamila yetu kama wizara ni kuhakikisha ifikapo mwaka   2030  kuwepo na food security na food security haiwezi kuwepo kama wakulima wetu wataendelea kulima kizamani”, amesema Mhandisi MDEKE 



Post a Comment

0 Comments