SUAMEDIA

SUA kushirikiana na wadau wa maji Mto Mbarali ili kulinda mazingira

Na Amina Hezron

Mbarali

Kutokana na uharibifu wa vyanzo vya maji na uoto wa asili uliofanyika kando kando  ya Mto Mbarali wa mkoani Mbeya, uliotokana na shughuli za kilimo na ufugaji, mradi wa Eflows unatarajia kuanzisha vitaru vya miti rafiki zaidi ya laki moja kwa ajili ya kupanda kandokando ya mto huo. 

Hatua hiyo imefikiwa baada ya Kiongozi wa mradi huo Prof. Japhet Kashaigili, kufanya ziara kandokando ya mto huo akiwa ameambatana na kiongozi wa bonde la mto Rufiji, Jumuiya za watumia maji na Viongozi wa skimu ya umwagiliaji ya Igomelo kwa lengo la kwenda kufanya tathimini katika eneo hilo


Prof. Japhet Kashaigili ambaye ni kiongozi wa mradi huo akizungumza na wadau hawako pichani wilayani Mbarali 

“Mradi pamoja na kufanya utafiti lakini pia tunataka kuwa sehemu ya kutatua baadhi ya changamoto na kutokana na hali ilivyo mbaya kwenye vyanzo vya maji vya mto huu na kandonkando ya mto hatua ya kwanza tunaanzisha vitalu vya miti ili ipandwe kwenye maeneo yote baada ya kupata ushauri wa aina ya miti inayofaa kutoka kwa wenzetu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania TFS Wilayani Mbarali” Alisema Prof. Kashaigili.

Amesema hawawezi kusubiri hadi mwisho wa utafiti wao ndio wafanye kazi ya kurekebisha makosa ambayo yanaonekana waziwazi hivyo lazima wapande miti rafiki ili kurudisha uoto wa asili.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Skimu ya umwagiliaji ya Igomelo Bi. Aurelia Kayombo, amemshukuru Mkuu wa Mradi huo kwa kufanya ziara hiyo kwa pamoja na kuwapatia elimu kuhusu sheria za mazingira na uhifadhi wa mito.

“Ziara hii imekuwa ya mafanikio makubwa na nikiri kuwa kuna uharibifu mkubwa umefanyika hatukuwa tunafahamu lakini kupitia ziara hii tumeweza kuona na sasa tunakwenda kuitisha kikao na wananchama wetu wote na kufanya ziara kama hii na ikiwezekana na viongozi wa wilaya nao wawepo ili tuweke makubaliano ambayo yatasaidia  kulinda mto huu muhimu” Alieleza Kayombo


                                          Eneo la Mto Mbarali likitiririka maji

Naye, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Watumia Maji wa Mto Mbarali (JUWAMBA) Bw. Siasa Shabani, amesema wamefanya kazi kubwa katika kutoa elimu na kuwakamata watu ambao wamekuwa wakivunja sheria na taratibu walizojiwekea ili kupunguza idadi ya watu wanaoharibu vyanzo vya maji lakini tatizo bado linaendelea.


Post a Comment

0 Comments