SUAMEDIA

Serikali yataka Mashirika na Taasisi za kidini kuwa na uwazi wa taarifa za mahesabu yao .

 

Na.Vedasto George

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan ameyataka Mashirika na Taasisi za kidini nchini kuwa na uwazi wa taarifa na mahesabu yao ili kuondoa changamoto mbalimbali zinazo jitokeza  pindi serikali inapotaka kukusanya kodi.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akitoa hotuba yake katika ufunguzi wa Mkutano  Mkuu wa  Jumuhiya ya Kikristo ambao umefanyika Kilakala Mkoani Morogoro.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Julai 8 katika Mkutano Mkuu  wa 31 wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania CCT Mjini Morogoro na kusema kuwa serikali inalazimika kuyatoza kodi mashirika ya kidini kutokana na baadhi ya taasisi hizo kuwa na mazingira ya kibiashara na sio kihuduma.



Aidha Mhe. Samia amesema serikali itaendelea kuheshimu misingi ya utawala wa sheria na haki za binadamu na kuongeza kuwa haitasita kuchukua hatua kali kwa viongozi na watendaji wa serikali wasio heshimu utawala bora na kukiuka haki za kibinadamu.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na baadhi ya  viongozi wa dini wakati akiwasili kufungua Mkutano  Mkuu wa   Jumuhiya ya Kikristo ambao umefanyika Kilakala Mkoani Morogoro.

Awali akizungumza katika Mkutano huo Mwenyekiti wa CCT Askofu Dkt. Alinikisa Cheyo amesema miongoni mwa majukumu wanayofanya kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali na Serikali ni shughuli za kijamii zenye lengo la kuimarisha haki, kujenga usawa wa kijinsia, na kuwajengea watu uwezo wa kuinua vipato vyao ili kuweza kujiletea maendeleo.

Kwa upande wake Mchungaji Agines Njeyo Mwenyekiti wa wanawake wa CCT ameoimba Serikali kufanya mabadiliko ya kisera, kisheria na utaratibu ambao utawawezesha watoto wa kike nchini kurudi kwenye mfumo rasmi wa kielimu baada ya kupata ujauzito.

Mkutano Mkuu wa 31 wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania CCT umeambatana na Uchaguzi Mkuu wa kuwachagua viongozi wapya wa Jumuiya hiyo ambao watahudumu kwa kipindi cha miaka minne.

Post a Comment

0 Comments