SUAMEDIA

 

Na Farida Mkongwe, Morogoro

Wafugaji wa kuku wameshauriwa kuhakikisha wananunua vifaranga kutoka kwenye mashamba ambayo yanatoa chanjo za awali ili kuepusha vifo vya vifaranga ambavyo vinasababisha hasara kwa mfugaji.

Wanafunzi wakimsikiliza Daktari Amina Ramadhani Issae muda mfupi kabla ya kuanza zoezi la kutoa chanjo

Ushauri huo umetolewa na Mtafiti kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA ambaye pia ni Daktari wa Mifugo Amina Ramadhani Issae wakati akizungumza na SUAMEDIA kwenye moja ya banda alilotembelea lililopo eneo la Nane Nane mjini Morogoro kwa ajili ya kutoa chanjo ya ndui ya kuku.

Daktari Issae akiwa ameambatana na wanafunzi wa mwaka wa kwanza wa Shahada ya kwanza ya Udaktari wa Mifugo kutoka Ndaki ya Tiba za Wanyama na Sayansi za Afya amesema chanjo ni jambo la msingi sana katika kuhakikisha kuku wanakuwa na afya njema.

“Mfugaji ni lazima ahakikishe anaijua historia ya shamba analonunua vifaranga kwa sababu kuna mashamba mengine yanauza vifaranga bila kuwapa chanjo za awali ikiwemo mareks, na pia ahakikishe shamba hilo halina historia ya magonjwa”, alisema Daktari huyo.

Aidha Mtafiti huyo kutoka SUA amewataka wafugaji kuzingatia mahitaji muhimu kwenye uchanganyaji wa chakula ili kuku waweze kupata virutubisho vyote vinavyohitajika pamoja na kuzingatia usafi wa banda na kuhakikisha banda linakuwa na hewa ya kutosha.


Daktari aliyeshika kuku akiwaelekeza wanafunzi namna ya kutoa chanjo ya ndui 

Kwa upande wao baadhi ya wanafunzi akiwemo Boniventure Bundara na Jumanne Ibrahim wamewashauri wafugaji kuwa na vyumba vya kutosha kwenye mabanda yao na kuwagawanya kuku kulingana na umri wao ili kuweza kuwapa chakula kwa kuzingatia hatua mbalimbali za ukuaji pamoja na kuzuia magonjwa ya kuambukiza.

Wanafunzi wa Shahada ya kwanza ya Udaktari wa Mifugo wakiwa na kuku tayari kwa ajili ya chanjo ya ndui





 




Post a Comment

0 Comments