SUAMEDIA

Wakulima wahimizwa kutumia Ghala la Mkulima kuongeza tija

 Na: Farida Mkongwe

Wakulima wamehimizwa kutumia Ghala la Mkulima linalosimamiwa na Maktaba ya Taifa ya Kilimo ya Sokoine (SNAL), iliyopo katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), ili kupata maarifa, ujuzi na teknolojia mbalimbali zitakazowasaidia kuongeza tija na faida katika shughuli zao za uzalishaji.

Wito huo umetolewa na Msimamizi wa Kitengo cha Maarifa na Huduma za Rejea katika maktaba hiyo, Bw. Jabir Jabir, kwenye viwanja vya Maonesho ya Wakulima ya Nanenane yanayoendelea katika Kanda ya Mashariki, mkoani Morogoro.

Amesema kilimo bora na chenye matokeo kinapaswa kufanyika kwa kuzingatia taarifa na maarifa sahihi kutoka kwa wataalamu.

Bw. Jabir amesema SNAL ina machapisho mbalimbali ambayo wakulima wanaweza kuyasoma kwa kufika maktabani au kuyapata kwa njia ya mtandao kupitia simu janja na vifaa vingine vya kidijitali.

“Kupitia Ghala la Mkulima, wananchi wanaweza kupata taarifa, maarifa  na mafunzo mbalimbali ya kilimo yaliyoandaliwa na wataalamu waliobobea katika sekta hiyo.

Ameeleza kuwa maktaba hiyo inawahudumia watu wa kada na viwango vyote vya elimu, huku machapisho yaliyopo katika Ghala la Mkulima yakiwa yameandikwa kwa lugha rahisi inayomwezesha mkulima kuelewa na kutumia maarifa hayo katika shughuli zake.

Amesisitiza kuwa matumizi ya taarifa na maarifa sahihi yatawasaidia wakulima kutambua mahitaji ya soko, kuchagua teknolojia bora na kuzalisha kwa tija.

Amesema hatua hiyo inaunga mkono kaulimbiu ya Maonesho ya Nanenane ya mwaka 2026 isemayo, “Tambua Soko; Ongeza Tija Kutekeleza Dira 2050.”




Post a Comment

0 Comments