Na: Farida Mkongwe
Wakulima na wadau wa sekta ya kilimo wamehimizwa kushiriki
mafunzo maalumu yaliyoandaliwa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA)
katika Maonesho ya Nanenane, ili kupata maarifa yatakayowasaidia kuendesha
kilimo kama biashara na kuongeza tija.
Akizungumza na SUA Media katika Maonesho ya Nanenane, Mkufunzi Msaidizi kutoka Idara ya Uchumi wa Kilimo na Biashara ya SUA, Anne Malando, amesema chuo kimeandaa mafunzo ya kila siku kwa wakulima na watu wengine wanaojihusisha na uzalishaji na biashara ya mazao ya kilimo.
Malando amesema siku za Agosti 1 hadi 3 zilitengwa kwa ajili
ya usajili wa washiriki, huku mafunzo yakipangwa kutolewa kuanzia Agosti 4 hadi
7, 2026, katika banda la SUA.
Ameeleza kuwa mafunzo ya Agosti 4 yanahusu mnyororo wa
thamani na sera, ili kuwawezesha wakulima na wafanyabiashara wa mazao kuelewa
namna ya kuongeza thamani katika kila hatua ya uzalishaji, usindikaji na uuzaji
wa bidhaa za kilimo.
Kwa mujibu wa Malando, mafunzo ya Agosti 5 yatahusu masoko
ya biashara ya kilimo, ambapo washiriki wataelimishwa kuhusu umuhimu wa
kutambua soko kabla ya kuanza uzalishaji na namna ya kutafuta masoko yenye
uhakika kwa mazao yao.
Amesema Agosti 6 mafunzo yataangazia uhasibu na usimamizi wa fedha katika biashara ya kilimo, ikiwemo namna ya kutumia mikopo kwa tija na kunufaika na huduma za taasisi ndogo za fedha zinazowahudumia wakulima.
Aidha, mafunzo ya Agosti 7 yatahusisha uhamasishaji wa
rasilimali na namna ya kuanzisha biashara za kimataifa, ili kuwajengea
washiriki uwezo wa kutafuta mitaji, kupanua biashara na kufikia masoko ya nje
ya nchi.
Malando amewashauri wakulima na wadau wengine wanaotembelea
Maonesho ya Nanenane kufika katika banda la SUA, kujisajili na kushiriki
mafunzo hayo ili kupata maarifa yatakayowawezesha kuendesha shughuli zao za
kilimo kwa ufanisi na faida zaidi.


0 Comments