Na: Farida Mkongwe
Mbegu ya mchicha lishe aina ya Amaranth ni miongoni mwa
mazao yanayooneshwa na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mafiga iliyo chini ya
Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) katika Maonesho ya Nanenane.
Akizungumza katika maonesho hayo, mwanafunzi wa kidato cha tatu katika mkondo wa amali ya kilimo, Mariam Abed, amesema mchicha huo una majani yenye virutubisho vingi vinavyosaidia kuimarisha afya ya mwili.
Mariam amesema aina hiyo ya mchicha ina uwezo wa kuvumilia
baadhi ya magonjwa ya mimea, yakiwemo magonjwa ya ukungu, hivyo kumsaidia
mkulima kupunguza uharibifu wa mazao shambani.
Ameeleza kuwa mchicha huo hukomaa ndani ya siku 35 hadi 40 baada ya kupandwa, hali inayomwezesha mkulima kuvuna kwa muda mfupi na kuuza mazao yake sokoni.
Ameongeza kuwa mchicha huo unafaa kutumiwa na watoto, wazee
pamoja na wanawake wajawazito kwa kuwa una virutubisho muhimu kwa mwili, huku
akiwashauri wakulima kulima mbegu bora ili kupata mazao yenye tija na lishe
bora.


0 Comments