SUAMEDIA

Jokofu la asili kuboresha maisha ya wajasiriamali Mikese, Morogoro

Na: Asifiwe Mbembela

 Wajasiriamali wadogo katika Soko la Lukole, Kata ya Mikese mkoani Morogoro, wameanza kunufaika na teknolojia ya jokofu la asili lililojengwa na watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia Mradi wa UNESCO-TWAS.

Teknolojia hiyo imelenga kuwasaidia wafanyabiashara kuhifadhi mazao yanayoharibika kwa haraka, yakiwemo nyanya, matunda na ndizi, ili kupunguza upotevu wa mazao baada ya kuvuna na kuyalinda yasiharibike kabla ya kuuzwa.

Wakizungumza wakati wa kukabidhiwa jokofu hilo, wajasiriamali hao wamesema awali walikuwa wakipata hasara kutokana na mazao kuiva na kuoza ndani ya siku chache endapo hayakuuzwa kwa wakati.

Mmoja wa wanufaika wa teknolojia hiyo, Bi. Zainabu Ally mwenye umri wa miaka 31, anayefanya biashara ya nyanya, amesema kuharibika kwa mazao kulikuwa kukisababisha kupoteza sehemu ya mtaji na wakati mwingine kulazimika kusitisha biashara.


“Tulikuwa tunapata wakati mgumu kwa sababu usipouza kwa wakati, nyanya zako zinaanza kuoza na unalazimika kuziuza hata kwa hasara,” amesema Zainabu.

Kiongozi wa Mradi huo, Dkt. Nuria Majaliwa, amesema teknolojia hiyo ina uwezo wa kuhifadhi nyanya na matunda kwa kipindi cha hadi wiki mbili, sawa na siku 14, hivyo kusaidia kupunguza upotevu wa mazao na hasara kwa wafanyabiashara.


Kwa upande wake, Kiongozi Mwenza wa Mradi, Dkt. Frida Nyamete, amesema jokofu hilo litawapa ahueni wajasiriamali kwa kuwa bidhaa zao zitaweza kuhifadhiwa kwa muda mrefu bila kuharibika, hata wanapolazimika kusafiri au kutokuwepo kwenye biashara kutokana na sababu mbalimbali.

Teknolojia hiyo inatarajiwa kuchangia katika kupunguza upotevu wa mazao baada ya kuvuna, kulinda mitaji na kuongeza kipato cha wajasiriamali wadogo katika Soko la Lukole na maeneo mengine yatakayofikiwa.








Post a Comment

0 Comments