Na: Ngolo Mboje – Morogoro.
Katika
kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimetoa fursa ya elimu ya
afya ya magonjwa yanayoambukiza na yasiyoambukiza na huduma ya vipimo bure bila malipo
kwa wanawake wa chuo hicho kwa lengo la kupata uewelewa kuhusu njia za
kujikinga na magonjwa mbalimbali.
| Baadhi ya Wanawake kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA wakiwa kwenye picha ya pamoja na wawezeshaji kwenye kongamano hilo. |
Akifungua kongamano la wanawake Prof: Faith
Philemon Mabiki kutoka Ndaki ya Sayansi Asilia na Tumizi (CoNAs) kutoka Chuo
Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) lililofanyika machi 4, 2026 katika Kampasi
ya Edwad Moringe chuoni hapo Mkoani Morogoro, amesema kuwa wanawake ni kundi
muhimu katika jamii na taifa kwa ujumla na nguzo muhimu katika kufanikisha
majukumu kiutawala.
Prof.
Mabiki ameishukuru Menejimenti ya SUA kwa kutoa fursa ya wanawake wa chuo hicho
kupima afya zao bila malipo kwa kuwa fursa hiyo itawasaidia wanawake kuwa sawa
kiafya na kumfanya mwanamke kufanya kazi vizuri na kwa ufanisi ili kuhakikisha Dira ya mwaka 2050 inafikia malengo.
Aidha kwa
upande wake Dkt. Elimwidimi Swai ambaye
ni Daktari Bingwa wa magonjwa ya uzazi na wanawake kutoka hospital ya Chuo
Kikuu cha Sokoine cha Kilimo amefundisha athari za magonjwa mbalimbali ya uzazi
ikiwemo Kansa ya shingo ya kizazi itokanayo na maambukizi ya virusi vya (HPV)
ambapo amewataka wanawake kupima afya zao mara kwa mara kwani magonjwa hayo
yanagundulika mapema na yanatibika kwa
haraka.
Kwa
upande wake Daktari bingwa wa magonjwa ya watoto SUA Dkt. Graca Chotamawe amesema kwa mujibu wa Shirika
la Afya Duniani (WHO), asilimia 70 ya watu millioni 41 wanakufa kwa mwaka kwa
magonjwa yasiyo ambukiza kutokana na kukua kwa teknolojia ya vyakula na ulaji,
na namna ya kuishi wakiwa katika shughuli za kila siku.
Aidha ametoa wito kwa wanawake kutambua namna
bora ya kuepuka magonjwa hayo ikiwemo kula vyakula asilia na kufanya mazoezi ya
mwili ili kupunguza vifo na umaskini nchini na kuwataka elimu hiyo ikawasaidie
kiafya na jamii zinazowazunguka.
Kwa
upande wake Bw. Faraja Kamendu ambaye ni Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi
(RAAWU) tawi la SUA amesema kuwa kongamano hilo ni chachu ya kuimarisha mtandao
wa wanawake wanaojitambua kwani wana uwezo wa kutimiza majukumu kwa ufanisi na
kwa ubora na kuahidi ushirikiano katika kila hatua ya maendeleo.
Hatua
hiyo pia inaonesha dhamira ya chuo katika kuunga mkono ustawi wa wanawake huku
kikielekea kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yatakayofanyika
tarehe 8 Machi 2026 ambayo kwa mwaka huu yamebeba kauli mbiu isemayo “Haki kwa Wanawake na Wasichana Msingi wa Maendeleo Jumuishi kufikia Dira 2050”.
MATUKIO KATIKA PICHA WAKATI WA KONGAMANO HILO.
| Daktari bingwa wa magonjwa ya watoto SUA Dkt. Graca Chotamawe akiwasilisha mada yake kwenye kongamano hilo. |
0 Comments