SUAMEDIA

Ubunifu na utafiti vyatajwa nguzo za maendeleo ya jamii

Na: Farida Mkongwe

Mshikamano wa kitaaluma, ubunifu na utafiti kati ya vyuo vikuu nchini umetambuliwa kuwa ni nguzo muhimu ya matokeo chanya katika nyanja za elimu na kuboresha maisha ya binadamu kwa kushughulikia changamoto zinazokabili jamii.

Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Uzamili, Utafiti, Uhaulishaji wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalamu ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Kongamano la Pili la Kisayansi la Muungano wa Vyuo Vikuu Vitano, Prof. Japhet Kashaigili kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), wakati akizungumzia malengo ya kongamano hilo linalofanyika mjini Morogoro.

Prof. Kashaigili amesema kongamano hilo limewakutanisha wataalamu na washiriki takribani 200 kutoka vyuo vikuu vitano vya ndani na nje ya nchi, ikiwemo SUA, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu cha Aga Khan, Chuo Kikuu cha Nelson Mandela, na Chuo Kikuu cha Simon Fraser cha Canada, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa makubaliano ya ushirikiano wa kitaaluma na utafiti yaliyofikiwa na vyuo hivyo.

Lengo la kongamano hili ambalo kwa mwaka huu limeratibiwa na SUA ni kubadilishana uzoefu na wataalamu, kuimarisha uwezo wa walimu na wanafunzi, pamoja na kuandaa machapisho ya pamoja ya tafiti yatakayosaidia kutafuta suluhisho la changamoto za kijamii,” amesema Prof. Kashaigili.

Aidha, amebainisha kuwa ubunifu unaozalishwa kupitia ushirikiano huo ni muhimu katika kuongeza tija ya kilimo, kuboresha huduma za afya na maji safi, sambamba na kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi kwa kujadili kwa kina hatua za kitaaluma na kiteknolojia zinazoweza kuchangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Kongamano hilo pia limekuwa fursa muhimu kwa watafiti chipukizi kuwasilisha tafiti zao na kujenga mitandao ya kitaaluma, hatua ambayo itasaidia kuendeleza mashirikiano haya kwa vitendo ili kuhakikisha tafiti zinazozalishwa zinakuwa na matokeo chanya kwa taifa na dunia kwa ujumla.

Kongamano la Pili la Kisayansi la Muungano wa Vyuo Vikuu Vitano mwaka huu limebeba kaulimbiu: “Zaidi ya Kuishi: Kujenga Jamii Shirikishi na Zinazostahimili Mabadiliko ya Tabianchi.”







Post a Comment

0 Comments