SUAMEDIA

Uandishi wa machapisho ya kisayansi wapewa kipaumbele SUA

Na: Ayoub Mwigune

Watafiti, wahadhiri na wanafunzi wa Shahada za Uzamili na Uzamivu wametakiwa kuzingatia uandishi wa machapisho ya kisayansi yenye ubora wa kimataifa, ili kuongeza tija katika tafiti na kuimarisha heshima ya vyuo vikuu vya Afrika kwenye majukwaa ya kitaaluma ya kimataifa.

Hayo yameelezwa katika mjadala wa kitaaluma ulioandaliwa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA)  kupitia Mradi wa NANO COM, uliolenga kuboresha uelewa wa uandishi wa kisayansi na ubora wa machapisho.

Awali, Prof. Gaymary Bakari, ambaye ni Kiongozi wa Mradi wa NANO COM nchini Tanzania na Naibu Rasi wa Ndaki ya Tiba ya Wanyama na Sayansi za Afya (SUA), amesema kuwa uandishi wa kisayansi ni ujuzi muhimu kwa kila mwanafunzi na mtafiti, kwani ndio kipimo cha kazi ya kitaaluma duniani.

“Kupitia mradi wa NANO COM, tunalenga kuwajengea uwezo watafiti na wanataaluma wetu ili waandike machapisho yenye ubora unaokubalika kimataifa. Hii itasaidia kuongeza machapisho kutoka SUA na vyuo vikuu vingine nchini,” amesema Prof. Gaymary.

Akichangia katika mjadala huo, Prof. Xin Zhao kutoka Chuo Kikuu cha McGill , Canada, amesisitiza kwamba ubora wa elimu na utafiti wa kisayansi ndio unaoamua maendeleo ya taifa. Amesema nchi zilizoendelea zimefanikiwa kwa sababu zimewekeza katika elimu, tafiti, na mfumo wa kuchapisha matokeo ya kisayansi kwa uwazi.

“Katika nchi nyingi zilizoendelea, wanafunzi hawawezi kuhitimu bila kuchapisha makala kwenye majarida yenye viwango vya juu, na wanasayansi hupandishwa vyeo kwa kuzingatia machapisho yao,” amesema Prof. Zhao.

 Amefafanua kuwa uandishi wa kisayansi unatakiwa kuwa wazi, sahihi na wenye ushahidi wa kisayansi. “Uandishi wa kisayansi sio kama wa riwaya. Unahitaji lugha iliyo wazi, hoja zenye uthibitisho, na matokeo yanayoweza kuthibitishwa. ChatGPT inaweza kusaidia kuhariri maandiko, lakini haiwezi kufanya majaribio ya kisayansi  inaweza kutoa takataka (garbage), hivyo chagua kwa busara,” ameongeza.

Prof. Zhao pia ametoa ushauri kwa wanataaluma na wanafunzi wanaoanza safari ya utafiti, akisisitiza kuelewa uzito na mchango wa tafiti zao kwa jamii sambamba na kuepuka kurudia tafiti zilizofanywa tayari na kufanya tafiti zenye ubunifu na mchango mpya katika jamii.







Post a Comment

0 Comments