SUAMEDIA

SUA yatekeleza mpango wa Serikali wa kukabiliana na UKIMWI na Magonjwa Sugu Yasiyoambukiza

 

Na: Hadija Zahoro

Katika kutekeleza azma ya Serikali ya kudhibiti na kutokomeza maambukizi ya virusi vya UKIMWI pamoja na Magonjwa Sugu Yasiyoambukiza (NCDs) mahali pa kazi, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeandaa semina elekezi kwa waelimisha rika ili kuwajengea uwezo wa kusaidia wenzao katika maeneo yao ya kazi na masomo.

Semina hiyo imefanyika Mei 31, 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Taasisi ya Elimu ya Kujiendeleza (ICE), Kampasi Kuu ya Edward Moringe na kuhudhuriwa na wanafunzi pamoja na watumishi kutoka Idara na Ndaki mbalimbali za Chuo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Semina hiyo kwa niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. Raphael Chibunda, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala, Bw. Peter Mwakiluma, amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha maambukizi mapya ya UKIMWI yanapungua hadi kufikia asilimia sifuri ifikapo mwaka 2030, sambamba na kutokomeza kabisa unyanyapaa na vifo vinavyotokana na magonjwa hayo.

Amesema SUA ni taasisi ya Serikali na kwamba imeingia katika mpango wa utekelezaji wa kampeni hiyo kuanzia mwaka 2021 hadi 2026 hivyo wapo katika mkakati wa kutimiza azma hiyo ya Serikali.

Ameongeza kuwa Serikali imewekeza kwa waelimisha rika katika taasisi, hivyo amewataka kuzingatia yale watakayoyapata katika semina hiyo elekezi kwa sababu wao ndiyo wanaokwenda kukutana na wenzao wenye changamoto  za kiafya kwa ajili ya kuwa nao karibu na kwenda kuwaelimisha namna gani ya kuishi na hata kutoa uelewa kuhusu huduma zinazotolewa na Serikali kupitia taasisi yao.

“Ni huduma ambazo zipo, kuna watu wenye changamoto hizo ambao wanapata huduma za aina zote za kimatibabu lakini hata za namna ya kuishi” amesema Bw. Mwakiluma.

Kwa upande wake, Bi. Hekima Titus Maketa, Mratibu wa Masuala ya UKIMWI na NCDs mahali pa kazi ambaye pia ni Afisa Utumishi wa ICE, amesema matarajio yao ni kwamba waelimisha rika hao watafikisha ujumbe katika idara na vitengo vyao sambamba na waelimisha rika wanafunzi kuwafikishia ujumbe wanafunzi wenzao.

Naye Abdulrahmani Ramadhan Jumaa pamoja na Joan Aloyce, wanafunzi wa mwaka wa tatu wa Shahada ya Sayansi ya Familia na Watumiaji, wamesema kuwa kupitia semina hiyo wamejifunza umuhimu wa kuhimiza utamaduni wa kupima afya, kufanya mazoezi na kula vyakula vyenye lishe bora. 





Post a Comment

0 Comments