SUAMEDIA

SUA yaipongeza RAAWU kwa kuendelea kutetea maslahi ya wafanyakazi

 

Na: Siwema Malibiche

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimekipongeza Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi ya Elimu ya Juu, Sayansi, Teknolojia, Ufundi Stadi, Habari na Utafiti (RAAWU) kwa kuendelea kuzungumzia na kusimamia maslahi ya haki na wajibu kwa wafanyakazi wa SUA huku kikiwataka  wafanyakazi kufuata taratibu, kanuni na sheria za utumishi wa umma ili kufikia malengo ya Chuo kwa maendeleo ya taifa.

Pongezi hizo zimetolewa Februari 18, 2025  na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo hicho anayeshughulikia Mipango, Utawala, na Fedha, Prof. Amandus Muhairwa wakati akifungua Semina ya Wanachama RAAWU Tawi la SUA na waajiriwa wapya iliyofanyika Kampasi ya Edward Moringe mjini Morogoro ambapo amesisitiza kuwa wafanyakazi wanatakiwa kutekeleza majukumu yao kwa weledi ili kuchochea maendeleo nchini.


Prof. Muhairwa amesema Chama cha Wafanyakazi RAAWU kinafanya kazi kubwa ya kutetea maslahi bora ya wafanyakazi hivyo amewataka wafanyakazi nao kuzingatia maslahi ya mwajiri na matumizi sahihi ya muda ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa RAAWU Taifa Bi. Jane Mihanji ameupongeza uongozi wa Chama cha Wafanyakazi RAAWU Tawi la SUA kwa kufanya kazi zenye ubora na kuwa mfano wa kuigwa kwa matawi yote nchini huku akisema kuwa anafurahi kuona viongozi wanatekeleza majukumu yao ipasavyo.


Pia amewataka wafanyakazi wote ambao wameshiriki katika semina hiyo kuambiana ukweli inapotokea mmoja wao anakiuka wajibu wake ili kuepuka kuunda makundi  yatakayoharibu weledi na uwezo wa kufanya kazi kwa ufanisi.


Kwa upande wake Mwenyekiti wa RAAWU Tawi la SUA Bw.Faraja Kamendu amesema wao kama viongozi wataendelea kusimamia maslahi ya wafanyakazi yatakayoleta tija huku akiwataka wafanyakazi kuendelea kushirikiana na kushikamana na amewakaribisha wafanyakazi wote waliopo SUA kujiunga na chama hicho ili waweze kufaidika na maslahi yanayotokana na utetezi wa RAAWU.

Semina hiyo imeandaliwa na Chama cha Wafanyakazi RAAWU Makao Makuu kwa kushirikiana na RAAWU Tawi la SUA ambapo kwa siku ya Jumanne Februari 18, 2025 imefanyika semina kwa wanachama wa Chama hicho na waajiriwa wapya wa SUA na Februari 19, 2025 ilikuwa ni semina kwa wafanyakazi wote wa SUA.







Post a Comment

0 Comments