SUAMEDIA

Mradi wa FoodLAND nchini waboresha ufugaji wa samaki wilayani Kilombero

 

Na: Ayoub Mwigune

 Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeendelea kuwaandaa wakulima mahiri katika sekta ya uvuvi na ufugaji wa samaki nchini, ili kusaidia kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.



Akizungumza wakati wa hitimisho la Mradi wa Chakula, Kilimo na Lishe (FoodLAND), Mhadhiri Mwandamizi na Mtaalamu wa Ufugaji na Uvuvi wa Samaki Dkt. Renalda Mnubi kutoka SUA amesema lengo kuu la mradi huo lilikuwa ni kuwawezesha wafugaji kwa kuwafundisha mbinu bora za ufugaji wa samaki pamoja na kuwapatia elimu ya vitendo, ili waweze kuzitumia katika mazingira yao ya kila siku.

 Dkt. Renalda amesema awali waliwapatia wakulima mafunzo ya nadharia na vitendo ambayo yaliwawezesha kufuga samaki, kuwavuna, na kuwauza, mafunzo ambayo yaliwafanya wakulima kutambua kuwa hawakuhitaji kutegemea samaki wa asili kutoka kwenye mito pekee, bali wangeweza kuwafuga wao wenyewe kwa ajili ya kuongeza kipato na kuboresha lishe ya familia zao.


 
Aidha katika kuhitimisha mradi huo ulioanza rasmi April 1, 2020 na kukamilika Februari 28, 2025,  wakulima walipata fursa ya kutembelea SUA na kujifunza kwa vitendo namna ya kufuga samaki kwa ufanisi, kutengeneza chakula bora cha samaki, na kujenga mabwawa ya kisasa.

Dkt. Renalda ameongeza kuwa uzalishaji wa chakula cha samaki kwa njia  binafsi uliwasaidia wafugaji kuondoa changamoto kubwa iliyowakumba katika ununuzi wa chakula cha samaki. 

"Uwezo wa kuzalisha chakula cha samaki wenyewe uliwaondolea utegemezi wa wafugaji kwa wauzaji wa chakula cha samaki, jambo ambalo liliongeza faida yao na kuboresha uzalishaji" amesema Dkt. Renalda. 

Kwa upande wao, Mariam Bakari na Festo Liguduliaka, wakazi wa Kijiji cha Mshikamano, Kata ya Mang'ula B, Halmashauri ya mji wa Ifakara mkoani Morogoro, ambao ni wanufaika na mradi huo, wameshukuru SUA kwa kuwapatia elimu hiyo muhimu ambayo imewawezesha kupata maarifa yaliyoboresha ufugaji wa samaki katika familia zao na kuinua hali yao ya kiuchumi.

Naye Mratibu wa Mradi huo kwa upande wa Tanzania, Prof. Suzan Nchimbi Msolla amesema kuwa lengo kuu la FoodLAND lilikuwa kuboresha lishe ya Watanzania kwa kuwapatia elimu kuhusu matumizi ya vyakula mbalimbali ili kujenga afya bora.





Post a Comment

0 Comments