SUAMEDIA

Zao la Kahawa kulimwa popote kama mkulima akizingatia mbegu bora, huduma na Elimu

 

Na loyce Sikira, Shabani Ramadhani,

Wananchi hasa wakulima nchini wametakiwa kujua elimu ya ulimaji wa zao la kahawa, jinsi ya kulihudumia zao hilo na namna ya upatikanaji wa mbegu bora ambapo kwa kuzingatia hayo upo uwezekano wa kulima zao hilo kwenye eneo lolote.

                        

Amebainisha hayo Bw. Godwin Rwezaula  Afisa Kilimo Mwandamizi  kutoka Ndaki ya Kilimo, Idara ya Mimea Vipando na Mazao ya Bustani katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA),  wakati akizungumza na SUA Media kuhusiana na elimu ya zao la kahawa lakini pia  uzalishaji wake kitaalamu ili kujiongezea kipato chao na cha Taifa kwa ujumla.

Amesema kuna aina kuu mbili za kahawa zinazozalisha SUA ambazo ni Robusta na Arabika na kati ya hizo kuna aina nyingine nyingi ambazo zimetoka katika Taasisi ya Utafiti Arusha na wao wanazifanyia utafiti ili kuzijaribu na kuona kiikolojia kama zinaweza kulimwa vizuri Mkoani Morogoro  

                                                                                                                                                                                  

Aidha Bw. Rwezaula amesema kwa kawaida kahawa hulimwa na kustawi vizuri sehemu za ukanda wa juu kama Kilimanjaro, Kigoma, Tabora, Mbeya pamoja na Mbinga na kwa Mkoa wa Morogoro zao hilo linaweza kulimwa vizuri katika maeneo ya ukanda wa juu kama vile Kinole, Matombo na Mkuyuni hivyo wao kama SUA kupitia tafiti wanazofanya wamegundua kuwa hata ukanda wa chini zao hilo linaweza kufanya vizuri endapo mkulima atazingatia namna bora ya ulimaji.

“Zipo aina bora za mbegu ya kahawa ambazo zina uwezo wa kustahimili katika maeneo ya ukanda wa chini hasa kwa Mkoa wa Morogoro hivyo mkulima akitambua aina hizo bora za mbegu ya kahawa na kufuata hatua kwa hatua namna bora ya uzalishaji wa zao hilo anaweza akazalisha kwa tija”, amesema Bw. Rwezaula.

                                        

Bw. Rwezaula ameongeza kuwa kati ya mambo ya msingi kwa mkulima anayeanza uzalishaji wa zao la kahawa ni lazima kuangalia Ikolojia aliyopo endapo inafaa kwa ajili ya zao hilo na baadaye kujua chanzo cha vipando ambavyo anahitaji kwa ajili ya kahawa hivyo kwa sasa wanashauri wapande kahawa bora kwa njia ya vikonyo ambapo kuna vitalu maalumu vikiwemo vya Serikali.







Post a Comment

0 Comments