SUAMEDIA

Timu ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Mradi wa HEET yatembelea Msitu wa Mafunzo Ifinga na Kampasi ya Mizengo Pinda

 

Na: Adam Maruma, 

Timu ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi - HEET kutoka Chuo Kikuu Cha Sokoine Cha Kilimo SUA, katika kutekeleza majukumu yake imetembelea msitu wa Mafunzo wa Ifinga uliopo Halmashauri ya Mji wa Madaba Mkoani Ruvuma pamoja Kampasi ya Mizengo Pinda iliyopo Mkoani Katavi.

                                    

Timu hiyo ikiongozwa na mkuu wa eneo hilo la mradi Dkt. Emmanuel Malisa na wajumbe wake Jumanne Habibu na Tryphone Ngoja, ilianza kazi kwa  kutembelea katika msitu wa Ifinga wenye hekta elfu 10 ambapo timu ilifika katika maeneo yaliyopandwa miti ambayo ni jumla ya hekta 1200, kitalu cha miche chenye miche 155,000 pamoja na eneo linalojengwa mnara utakaotumika kugundua uwepo wa moto katika shamba.

Dkt. Malisa amesema kazi ya eneo hilo la mradi ni kufuatilia, na kutathmini maendeleo ya mradi kuelekea kwenye ufikiwaji wa lengo kuu, na hivyo, wanakusanya taarifa mbalimbali, kuzichakata, na kuandika taarifa itakayopitishwa kwenye vikao mbali mbali vya Chuo, na baadae kuwasilishwa Wizarani (Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia).

                            

Mkuu huyo wa eneo la mradi la ufuatiliaji na tathmini amesema timu imejifunza mambo mbali mbali ikiwa ni pamoja na kuona namna Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo - SUA, kinavyoendesha msitu huo mkubwa wa mafunzo ulioanzishwa mwaka 2018, ambao hakika ni wa msaada mkubwa kwa wanafunzi pindi wanapokua katika mafunzo ya vitendo.

Dkt. Malisa ameongeza kuwa msitu huo umekuwepo kabla ya ujio wa Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi - HEET, ukiwa chini ya Ndaki ya Misitu, Wanyamapori na Utalii lakini ujio wa mradi  wa HEET umeongeza nguvu ya uendelezwaji wa msitu ambapo kwa msimu wa mwaka 2023/24 mchango wa mradi wa HEET umeanza kuonekana kwa ongezeko la ukubwa wa shamba lililopandwa miti toka hekta 278 msimu uliotangulia (2022/2023) hadi hekta 312,  ambalo ni ongezeko la hekta 34, ambayo ni sawa na asilimia  12.

Ameongeza kuwa katika kitalu cha kuaandaa miche kuna miti 155,000 (laki moja na hamsini na tano elfu) ambayo ingepandwa shambani ingetosha kupanda eneo lenye ukubwa wa hekta 140, na hivyo hekta hizi zikiongezwa kwenye zile hekta 34 zilizopandwa mwanzo, itafanya ongezeko hilo kuwa asilimia 63 ambayo ni mchango wa Mradi wa HEET katika msitu huo.

                        

Dkt. Malisa amesema lengo la mwanzo lilikuwa ni kupanda hekta 500 lakini mpaka sasa hekta zilizopandwa ni 312 na hivyo kasi ya upandaji inatakiwa kuongezwa na kwamba timu yake itajaribu kuainisha changamoto na namna ya kuweka sawa ili zoezi liendelee vizuri. “…na hili ndilo lengo kuu la ufuatiliaji; ni kutoa ‘early warning’ ili mradi uweze kubakia kwenye mstari sawasawa na mpango wake ulioainishwa kwenye andiko la mradi”.Amesema Dk. Malisa.

Amezitaja baadhi ya sababu zinazopelekea upandaji wa miti  kuwa chini kiwango cha hekta 500 ambazo zilikuwa ndio lengo upandaji wa shamba hilo kwa mwaka kuwa ni changamoto ya usafiri ambao ungetumika kubeba vibarua kutoka katika makazi yao hadi shambani, usafiri wa kubeba miche toka kitaluni hadi shambani, na usafiri wa wasimamizi wa msitu. Hayo yamepelekea kusia mbegu katika kitalu mwezi Oktoba badala Julai ambao ndio muda unaoshauriwa kitaalam, hali ambayo imepelekea kushindwa kufikia lengo ka hekta 500.

                            

Katika hatua nyingine, timu hiyo ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi - HEET imetembelea Kampasi ya Mizengo Pinda ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo iliyopo mkoani Katavi.

Timu hiyo imekutana na wafanyakazi na baadhi ya wanafunzi wa kampasi hiyo kwa lengo la kutaka kujua uelewa na ushiriki wao katika mradi wa HEET, na kujadili changamoto na tahadhari zilizopo kuhusu mradi.

Dkt. Malisa amesema, uelewa wa wafanyakazi kuhusu mradi wa HEET ni mkubwa hususan kwenye masuala ya jinsia na wafanyakazi wameonekana kuridhishwa na ushirikishwaji wao katika mradi. Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Rasi (Mipango, Utawala na Fedha) Profesa Jeremiah Makindara amesema katika Kampasi hiyo tayari limeanzishwa Dawati la Jinsia na kuna Kamati ya Uratibu wa Mradi wa HEET.



Kwa upande wake, Bw. Gabriel Mruma ambae ni mfanyakazi wa Chuo katika Idara ya Miliki, amesema yeye alikua mmojawapo wa walioshiriki kikamilifu katika zoezi la kufanya tathmini ya athari za kimazingira na kijamii za mradi, pamoja na zoezi la kutambua maeneo ambako majengo mbalimbali yatajengwa chini ya Mradi wa HEET. Kupitia kikao hicho, timu ilipokea pia taarifa kuhusu matarajio ya jamii inayozunguka Chuo kuhusu mradi ikiwemo kupatikana kwa ajira na kipato kwa makundi mbalimbali kama mama lishe, vibarua na wamiliki wa nyumba za kupanga.

Kwa upande wa wanafunzi, Dkt. Malisa amesema kuwa bado kuna changamoto ya uelewa kuhusu mradi huo. Hata hivyo, wajumbe wa Timu hiyo, Bw. Habibu Jumanne na Tryphone Ngoja walitumia fursa hiyo kuwapa maelezo kuhusu mradi na namna mradi utakavyoboresha baadhi ya miundombinu katika Kampasi hiyo.

Katika kuhitimisha vikao hivyo viwili, wajumbe wa Timu ya Ufuatiliaji na Tathmini walishauri uwepo wa utaratibu maalum wa kupashana Habari kuhusu Mradi wa HEET katika Kampasi hiyo kwa namna ambayo hata wafanyakazi au wanafunzi ambao hawakushiriki vikao mbalimbali wataweza kupata taarifa kuhusu yaliyojiri. Aidha, wanafunzi wameshauriwa kuwa wanatembelea tovuti ya Chuo ili kujipatia taarifa mbalimbali za Chuo ikiwa ni pamoja na za Mradi wa HEET.

 












KATIKA VIDEO

Post a Comment

0 Comments