SUAMEDIA

Rais Samia kufanya ziara mkoani Morogoro

 

Na: Ayoub Mwigune

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajia kufanya ziara ya kikazi ya siku tano mkoani Morogoro kuanzia tarehe 2 hadi 7 Agosti 2024, kwa lengo la kutembelea na kukagua  miradi ya maendeleo sambamba na  kuzungumza na wakazi wa mkoa huo.

Hayo yameelezwa Julai 30, 2024 na Mkuu wa mkoa wa Morogoro Adam Malima wakati akizungumza na waandishi wa  habari ofisini kwake kuhusu ziara hiyo.

Malima  amesema Rais Samia ataanzia ziara yake katika wilaya ya Gairo ambapo atakagua miradi mbalimbali sambamba na kuzungumza na wananchi wa wilaya hiyo ambapo Agosti 7, 2024  atazungumza na wakazi wa Morogoro katika uwanja wa Jamhuri uliopo Manispaa ya Morogoro.

Mkuu huyo wa mkoa amewaomba wakazi wa Morogoro kujitokeza kwa wingi kumpokea na kumsikiliza Mhe. Rais kwani ujio wake katika mkoani humo ni utekezaji kwa vitendo wa namna ambavyo Serikali ya Awamu ya Sita ilivyoweza kuwekeza katika miradi mbalimbali ya kimaendeleo kama maji, elimu na usafirishaji.

Kwa upande wao baadhi ya wakazi wa Mkoa huo akiwemo Bw. Shaban Ramadhan na Flavian Nofred wamesema ziara ya Mhe. Samia itatoa  mwangaza katika sekta ya kilimo kwani mkoa wa Morogoro umekuwa ukifanya vizuri katika sekta hiyo.

Wamesema kuwa ziara hiyo ya Rais Samia itawapa nafasi wakulima kuweza kusikia malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kilimo huku wakitoa wito kwa wakazi wa Morogoro kujitokeza kwa wingi ili kumsikiliza Mhe. Rais.

Post a Comment

0 Comments