SUAMEDIA

Wazalishaji wa Mvinyo watakiwa kuzingatia ubora na usalama wa mtumiaji

 Na: Asifiwe Mbembela

Washiriki wa semina ya kitaalamu ya uzalishaji wa mvinyo nchini wameaswa kuwekeza muda  wao katika kujifunza namna nzuri ya kuandaa na kuzalisha divai bora ili iweze kushindana na bidhaa kama hizo ambazo zinazalishwa na mataifa shindani.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Shahada za Uzamili, Utafiti Uhauwilishaji wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalamu Prof. Japhet Kashaigili wakati akifungua mafunzo hayo yaliyoandaliwa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kwa ushirikiano na TARI-MAKUTOPORA, Kiwanda cha Utengenezaji wa Mvinyo cha Alkovintage na Ushirika wa Wakulima wa Zabibu na Masoko (UWAZAMAM) yaliyofanyika Jijini Dodoma.

Prof. Kashaigili amesema uzalishaji wa mvinyo una mahitaji makubwa kwa watumiaji wa ndani na nje ya nchi hivyo kama kutakuwa na uzalishaji wenye kuzingatia viwango vizuri, mvinyo wa Tanzania utaweza kuwa soko hata nje ya mipaka ya nchi tofauti na hali ilivyo kwa sasa.

“Ukipita kwenye maeneo mengi hapa Dodoma, huwa naona chupa mbalimbali za mvinyo, lakini nyingine zina nembo ya nje sasa unajiuliza tutaweza kushindana nao kwa ubora na bei, sasa kama wazalishaji wa ndani ni lazima tuambiane ukweli kuwa tujikite kwenye kuzalisha mvinyo wenye ubora ambao utauzika hata nje ya nchi bila shida”, alisema Prof. Kashaigili.

Ameongeza kuwa uzalishaji wa mvinyo kwa miaka ya sasa ni chanzo kikubwa cha mapato hivyo uwekezaji mzuri katika uzalishaji utaongeza kipato pamoja na kuongeza mtandao wa fursa (networking) baina ya wazalishaji na wataalamu.

Mtafiti Mwandamizi kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI - MAKUTUPORA) Felista Joseph Mpore akiongea katika semina hiyo pamoja na kuhimiza umuhimu wa kuchagua zabibu bora wakati wa uandaaji pia ameeleza namna sukari ilivyo na athari chanya ama hasi katika kuufanya mvinyo kuwa mzuri.

Mtafiti Mwandamizi kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI - MAKUTUPORA) Felista Mpore akitoa mafunzo katika semina hiyo


Kwa upande wake, Prof. Bendantunguka Tiisekwa Mwezeshaji katika semina hiyo akiwa ni Mkurugenzi wa Kituo cha Mafunzo ya Biashara na Usindikaji wa Chakula, ameeleza kuwa ili miradi ya wazalishaji wa divai iweze kudumu na kuwa na tija ni umuhimu shughuli zao zizingatie matakwa na sheria na kanuni zilizopo, ikiwemo usalama wa mlaji.

Prof. Bendantunguka Tiisekwa akiwasilisha mada katika semina hiyo kuhusu masuala ya sheria

Mafunzo kwa wazalishaji wa mvinyo yanafanyika chini ya Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) ukiwa ni mkakati wa Chuo kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuongeza uzalishaji wa mvinyo kupitia viwanda, elimu, ujuzi na maarifa mbalimbali yanayoendelea kutolewa na SUA.

Picha mbalimbali za washiriki wa ya wazalishaji wa mvinyo (picha zote na Asifiwe Mbembela)










Post a Comment

0 Comments