SUAMEDIA

SUA kuendeleza mazingira jumuishi na salama kwa wanafunzi wenye mahitaji Maalumu

 

Na: Josephine Mallango 

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeendelea na juhudi za  kuweka mazingira jumuishi na  salama kwa wanafunzi wenye mahitaji Maalumu ili kuhakikisha wanafikia malengo yao .

                           

 Akizungumza na SUA Media Mratibu wa Kitengo cha  Elimu Jumuishi na Mahitaji maalum chini ya mradi wa HEET Dkt. Thabita Lupeja amesema wanaendelea kutoa Elimu kwa wanafunzi wote wenye mahitaji na wasio na mahitaji maalum ili kila mtu ajisikie kuwa na haki sawa.

 Dkt. Lupeja amesema katika zoezi la upimaji macho na masikio, changamoto kubwa iko katika  masikio ambapo imekuwa ni vigumu watu kupokea matokeo ya kuwa na changamoto ya usikivu kutokana na hali hiyo kuwakuta wakiwa watu wazima .

 "Zoezi la upimaji linaloendelea limeanzia Mazimbu na litafika mpaka Kampasi ya Edward Moringe, limeambatana na watalaam wakiwemo kutoka UDSM  ambao Wana vifaa maalum vya kupimia changamoto kubwa ni watu kukubali  hasa kwenye tatizo la kusikia kwa kuwa linawakuta wakiwa wakubwa lakini  zoezi hilo limeambatana pia na watalaamu wa  kutoa ushauri kwa namna mtu anavyokutwa  na kiwango cha tatizo  wanamshauri  namna ya kuendelea  kulinda usikivu na kuendelea na maisha ya kawaida" , amesema Dkt. Lupeja.

 Mratibu huyo wa Kitengo cha  Elimu Jumuishi na mahitaji amesema wametoa mafunzo kwa wanafunzi wasio na changamoto ili waweze kuwa na utu wa  kuwasaidia wenzao wenye changamoto.

 "Kuna mwanafunzi mmoja  mwenye mahitaji maalumu amelalamika kujibiwa vibaya na mwenzake alipomuomba msaada wakiwa kwenye foleni wakati anaona wazi mwenzie ana changamoto, hiyo ni miongoni mwa baadhi ya matukio yaliyochochea mradi kuona hata wanafunzi wasio na changamoto wanatakiwa kupata Elimu ya kuwa msaada kwa wenzao kwa kuwa  changamoto au ulemavu siyo kipimo cha mtu kutokuwa na uwezo", amesema Mratibu huyo.

 Nao wanafunzi waliopima na kuzungumza na SUA Media wamekishukuru Chuo Kikuu cha Sokione cha Kilimo kwa kufanya zoezi la upimaji bure kwa madai  kuwa vipimo hivyo vina gharama kubwa na wao wasingeweza kumudu gharama hizo.

 "Vipimo hivi ni bei mbaya hasa usikivu masikio hii fursa Chuo wametupatia nawaomba wanachuo  wenzangu wajitokeze kupima kujua ugonjwa mapema kuna faida unatibu kuliko kuchelewa  inatumia muda mrefu kidogo kutatua changamoto",  amesema Onike Joseph mwanafunzi wa SUA.

 Zoezi la upimaji wa baki ya uoni na usikivu linaendelea Kampasi ya Edward Moringe kwa siku 2 ambazo ni Mei 9 na Mei  10, 2024 na linafanyika  bure kwa wanafunzi wote likiwa na lengo la kuwabaini wanafunzi wenye changamoto ili kuwasaidia kufikia malengo kwa kuwekewa mazingira  salama na jumuishi ili waendelee kusoma  pasipo kuathiri masomo yao na kuwa na  haki sawa kwa  wanafunzi wote.

  







Post a Comment

0 Comments