SUAMEDIA

Mkoa wa Morogoro salama kwa Utalii

 Na :Josephine Mallango 


Mkoa wa Morogoro umetajwa kuwa ni mkoa salama kwa utalii ambao una nyongeza ndani yake ya kuwa na njia za utalii na maeneo mbalimbali ya  vivutio vya utalii vilivyomo mkoani humo.                                                                 


Hayo yameelezwa na Mkuu wa Mkoa huo Adam Malima hivi karibuni wakati akifungua  mafunzo ya wanahabari zaidi ya 30 ambao  pia amewateuwa kuwa  wanakamati wa hamasa ya utalii mkoani Morogoro.


Akizungumza katika mafunzo hayo yaliyoandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari Tanzania (TAMPA) kwa kushirikiana  na TANAPA, Malima amewataka wanahabari kuendelea  kutangaza vivutio vyote vilivyomo mkoani Morogoro sanjari na wawekezaji kuja kuwekeza hotel za kitalii ndani ya mkoa huo.

                                


"Mkoa wa Morogoro umebarikiwa ni Mkoa wenye vivutio na vile vile  watalii wanapita kwenda kwenye utalii katika mikoa mingine na wenyewe Morogoro una hifadhi tatu Udzungwa , Mwalimu nyerere na  Mikumi ambayo ina mpaka mnyama Simba kipenzi cha  watalii wengi, bado kuna vivutio ikiwemo chemchem ya maji moto Kisaki, vinyonga wa kipekee  katika hifadhi asili ya Uluguru ila tujuwe wazi uwepo wa utalii pekee hautoshi tuanze na hamasa kutoka kwa wanahabari na wawekezaji wajitokeze kujenga hotel katika maeneo hayo ya utalii ikiwemo Mikumi, Ruaha , Kilombelo na  Morogoro", amesema Malima.


Kwa upande wake Afisa Maliasili na Utalii mkoa wa Morogoro Joseph Chuwa amesema mkoa huo uko katikati na una vivutio vingi vya utalii vya kipekee ambavyo bado havijatumika ipasavyo katika kufungua utalii ambao utaongeza ajira na mapato kwa mkoa na Taifa.


"Bado mkoa haujatumia vivutio vilivyopo katika kujikwamu , kuna vivutio ikiwemo  Mazimbu makazi ya zamani ya waafrika Kusini waliopigania Uhuru, kuna makaburi kule, waafrika Kusini wanahitaji kila mwaka pawe vile vile, Mandera aliishi pale kwenye harakati akiwa bondia , utalii huo upo Morogoro pekee, waandishi  tangazeni vema utalii katika kuleta fursa mpya ndani ya mkoa wetu", amesema  Chuwa.


Kwa upande  wake Rais wa Chama cha Waandishi wa Habari Tanzania (TAMPA) Simon Mkina amesema wamekutana na waandishi wa habari Morogoro kuwapa mafunzo juu ya kuandika habari za vivutio vya utalii  Morogoro ambavyo vipo na havijulikani kwa kuwa utalii ni moja ya kichocheo za uchumi.


Mkufunzi wa mafunzo hayo kutoka Chuo cha Taifa cha Utalii Kampasi ya Temeke  Amiri Abdi amesema utalii ni moja ya sekta inayotoa ajira kwa vijana na kwamba takwimu kutoka kwa Mtakwimu Mkuu na Benki ya Tanzania zinaonesha kuongezeka kwa watalii nchini kutoka milioni 1.5 mwaka  2022  mpaka milioni 1.8 mwaka 2023.


Mkufunzi huyo ameongeza kuwa mpango wa Serikali wa sasa chini  ya Rais Samia Suhuhu Hassan ni kufikia wataliii milioni 5 ifikapo 2025 , hivyo juhudi za mkoa wa Morogoro zinazoendelea ikiwemo Mkuu wa mkoa wa Morogoro Adam Malima kukubali kufufua utalii na kutangaza vivutio vilivyopo zinashabihiana na kasi ya taifa ya  mwaka 2025.







Post a Comment

0 Comments