SUAMEDIA

Elimu kuhusu masuala ya kuzingatia kazini hata kustaafu ni muhimu kwa Wafanyakazi

 

Na:Tatyana Celestine      

Katika kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Mei Mosi Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi za Elimu ya Juu Tanzania (THTU) Tawi la SUA wamefanya Kikao cha Mwaka pamoja na kutoa mafunzo mbalimbali kwa wanachama wake lengo ikiwa ni kuwakumbusha masuala muhimu ya kuzingatia wawapo kazini hata mara baada ya kustaafu.

                          

Katika kikao hicho wanachama wamepata kujifunza mambo yahusuyo Afya, jinsi ya matumizi na kuweka akiba, Mafao na kikokotoo lakini pia namna bora ya kufuatilia haki zao kwa kutambua sheria za msingi za chama hicho pamoja na kufahamishwa namna watakavyoweza kupata msaada wakipata changamoto wawapo kazini.

                                 

Akizungumza na SUAMEDIA wakati wa kikao hicho Dkt. Erhard Kapilima kutoka Kurugenzi ya Huduma za Afya Hospitali ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA ambaye pia ni mtoa mada kuhusu Afya amewaasa wafanyakazi wote kujua namna bora ya kuishi,  kuzingatia kufanya vipimo mara kwa mara pamoja na kupata matibabu stahiki kwani asilimia kubwa ya wafanyakazi kwasasa wanafariki kutokana na magonjwa yasiyoambukiza kama vile Shinikizo la damu (Presha), Kansa, Msongo wa Mawazo, Kisukari tofauti na miaka ya zamani.

                              

Dr. Kapilima ameongeza kuwa mtindo wa maisha wa sasa umesababisha watu wengi kuona hayo ndio maisha bora lakini kwa upande wa afya ni tatizo kubwa kwani wamekuwa hawazingatii vyakula sahihi, wanabobea katika matumizi ya pombe, uvutaji sigara, na Shisha ambapo vyote hivyo sio salama kwa afya  ya mwanadamu hivyo wanatakiwa kujenga tabia ya kufanya mazoezi, kula vyakula vya asili na kuachana matumizi ya vilevi ili kuepuka magonjwa yasiyo ya lazima,

Kwa upande wake Afisa Sheria wa Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi za Elimu ya Juu Tanzania (THTU) Taifa Wakili Mohamed Kusekwa amesema kuwa wafanyakazi wengi hawana taarifa sahihi zinazohusu haki zao wawapo kazini wengine kufikia kukubali makosa wanapokosea kwa kuambiwa watasamehewa ili hali katika sheria za kazi hakuna msamaha  bali watapewa adhabu kulingana na kosa alilotenda hata kama akikubali kosa husika.

                                 

Wakili huyo amebainisha kwamba kila mfanyakazi anatakiwa kujua sheria na taratibu za Chama chake cha wafanyakazi alichojiunga lakini pia kutofanya maamuzi ya kisheria bila kupata ushauri unaofaa kutoka kwa wanasheria wao nao waweze kuwasaidia pindi waingiapo kwenye migogoro na waajiri wao kufanya hivyo itawasaidia kupata haki bila kikwazo.

Naye Dkt. Prisila Mkenda Mhadhiri SUA kutoka Idara ya Sayansi ya Viumbe Hai ambaye pia ni mwanachama wa THTU alipotakiwa kuzungumzia faida  ya kikao hicho kupitia chama chao amesema utaratibu wa Chama chao  kutoa elimu ni suala mtambuka kwani inamfanya mfanyakazi kutambua alikotoka alipo na anapoelekea katika nyanja zote ikiwemo Afya, Stahiki za uzeeni, sheria, namna ya kuweka akiba na matumizi ya fedha wawapo kazini.

 Ameongeza kuwa kwa upande wa Afya kwa kuwa wao wamekuwa na maisha yasiyo na mazoezi ya kuutosha mwili kwa kwenda ofisini kwa gari, wanakula na kunywa wawapo ofisini na baadae kurudi nyumbani kwa kutumia usafiri uleule kwa tathmini hiyo ni dhahiri hawana mazoezi ya kuutosha mwili hivyo ushauri walioupata ni muhimu kwa kila mmoja wao kuuzingatia ili wawe na afya bora sasa na hata baada ya kustaafu.

                                

              
             

             

               

              

              



 

        


          


           
                                   

Post a Comment

0 Comments