SUAMEDIA

Utafiti wa afya na mtiririko wa maji ya Mto mbarali utasaidia Viongozi kufanya maamuzi sahihi.

 Na: Calvin Gwabara - Mbarali

Serikali Wilayani Mbarali imekipongeza Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) pamoja na Baraza la Taifa la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa jitihada zao za kusaidia kurejesha uoto wa asili kwenye vyanzo vya maji pamoja na kufanya utafiti na kutoa matokeo ambayo yataisaidia Serikali kufanya maamuzi sahihi.

Mkuu wa Wilaya ya Mbarali Mhe. Kanali Denis Mwila wakati akifungua warsha ya kutoa matokeo hayo.

Hayo yameelezwa na Mkuu wa Wilaya ya Mbarali Mhe. Kanali Denis Mwila wakati akifungua warsha ya kutoa matokeo ya utafiti wa Mradi wa usimamizi endelevu wa madakio ya maji kupitia tathimini ya kuimarisha mtiririko wa maji kwa mazingira na utekelezaji wake katika kulinda Ukanda wa Magharibi mwa Bahari ya Hindi na athari za shughuri za kibinadamu Tanzania (EFLOWS) iliyofanyika Wilayani humo Mkoani Mbeya.

 “Kuna athari kubwa ya kiusalama ambayo inaonekana kuja kwa juu kwa sasa ya uharibifu wa mazingira lakini ukiangalia kwa makini na kwa mujibu wa vitabu kadhaa nilivyosoma inaonekana vita ya tatu ya dunia itakuwa ni vita ya maji na hii imeanza kudhihirika kwenye maeneo mbalimbali na mfano mzuri ni eneo la mto Nile na hata ninapopita kwenye wilaya yangu kuongea na Wananchi swala la maji ndio kilio kikubwa” alieleza Mhe. Kanali Mwela.

Amesema matokeo hayo mazuri ya kina na kisayansi ya utafiti ya Mradi wa EFLOWS watayapitia vizuri na kuyatumia katika kutekeleza mipango mbalimbali ya uhifadhi kupitia mapendekezo yaliyotolewa ili kusaidia kuhifadhi vyanzo vya maji na mazingira kwa manufaa mapana na Taifa kwa kuwa vyanzo vya maji vilivyo nyanda za juu kusini ndivyo vinavyotegemewa kutiririsha maji yake kwenye mto Ruaha mkuu na hatimae Bwawa la Kidatu na Mwl. Nyerere

Amesema kuwa kumekuwa na uelewa kidogo wa jamii na baadhi ya viongozi katika masuala ya uhifadhi wa mazingira na vyanzo vya maji ndio maana Serikali inapochukua hatua za kuzuia shughuli fulani za kibinadamu kwenye maeneo muhimu ya vyanzo vya maji na hifadhi huzuka malalamiko mengi ambayo chanzo chake kikubwa ni ubinafsi wa watu wachache usiojali maslahi ya watu wengi na Taifa.

“Nyanda za juu wasipotunza vyanzo vya maji na kufuata sheria za uhifadhi wa mazingira Mradi mkubwa wa kufua umeme wa Bwawa la Mwl Nyerere hautafanya kazi na hivyo kusababisha nchi kukosa umeme wa kutosha kuendesha Viwanda, Treni ya Mwendokasi (SGR) na shughuli zingine za jamii zitakwama maana nishati hii ni muhimu kwa kila mtu” alieleza Kanali Mwela.

Mhe. Kanali Mwela amepongeza kazi hiyo kubwa ya utafiti iliyofanywa na SUA kwa kushirikiana na NEMC katika kufanya tathimini ya mtiririko wa maji kwenye mto Mbarali ambao unachangia maji yake kwenye Mto Ruaha mkuu na hatimae kuelekea Bwawa la Mwl. Nyerere na kwamba matokeo hayo yanasaidia kuonesha vizuri hali halisi ya vyanzo vya maji na mtiririko wake na nini kifanyike.

Kwa upande wake Mtafiti Mkuu wa Mradi wa EFLOWS kutoka (SUA) Prof. Japhet Kashaigili amesema katika kipindi cha miaka miwili ya utafiti huo tathimini ya kina imefanyika kuangalia hali ya vyanzo vya maji vya mto Mbarali, Afya ya Mto, Maumbile ya mto na uoto wake kupitia wataalamu waliobobea nchini kwenye nyanja hizo kutoka taasisi mbalimbali nchini na wananchi wa maeneo hayo hususani Jumuiya za watumia maji.

“Wakati tunakuja kutambulisha mradi tuliitana wadau wote wa maji wa mto Mbarali na tukawaeleza malengo ya ujio wetu wa utafiti huu na wengi wenu mlishiriki pia wakati wa utafiti wenyewe katika kipindi chote na baada ya kukamilisha kuchakata matokeo ya yale tuliyoyaona kisayansi sasa tumeona ni vyema kurudi tena kwenu kuwapatia mrejesho ili kwa pamoja tujue tunawezaje kutumia matokeo hayo kwa pamoja kusaidia kulinda vyanzo vya mito yetu na mazingira kwa faida ya Taifa” alieleza Prof. Kashaigili.

Aliongeza kuwa“ lengo la pili ni kujadili hatua za kuchukua ili kufikia malengo ya usimamizi na mpango wa utekelezaji na kuainisha wadau, majukumu, mpango na ushirikiano ili sote kwa pamoja tukubaliane cha kufanya na kushiriki kikamilifu maana tunategemeana na tunakwenda na usemi uleule kuwa ukitaka kufika mbali nenda na wenzako ila ukitaka kwenda haraka nenda peke yako na sisi lengo ni kufika mbali hivyo lazima twende pamoja”.

Prof. Kashaigili amesema takwimu na sampuli zilikusanywa kwenye maeneo manne waliyoyateua kupitia vigezo mbalimbali na zoezi hilo lilifanyika wakati wa kiangazi wakati kina cha maji mtoni kiko chini na wakati wa masika kipindi mto umejaa maji kuanzia mwanzo mwa mto katika eneo la Wilaya ya Wanging’ombe na Mbarali ambako unaishia na kumwaga maji yake kwenye mto Ruaha mkuu.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Tafiti za Mazingira kutoka (NEMC) Dkt. Menan Jangu amesema Baraza linajukumu kubwa la kuhakikisha miradi mikubwa inayoanzishwa inafikia malengo kwa kupata mahitaji yanayohitajika kwa  kupitia utunzaji wa mzingira na vyanzo vya maji.

Amesema ni wazi kuwa Mazingira, Ikolojia, bioanuai na huduma zinazopatikana zinaendelea kupata changamoto kubwa kutokana na ongezeko la watu, ongezeko la mahitaji na kwamba changamoto hizo zisipopatiwa ufumbuzi rasiliamali nyingi zinaweza kutoweka hususani mtiririko wa maji ambao ni uhai wa Wanyamapori, Binadamu na Miradi mikubwa ya uzalishaji wa nishati nchini.

“Utekelezaji wa utafiti huu ni moja ya malengo ya NEMC katika kuhakikisha kunakuwepo na tafiti nzuri na za kina ambazo zinafanywa nchini katika eneo la mazingira ili kupata matokeo na suluhu za kisayansi ambazo zitasaidia kuhifadhi mazingira na vyanzo vya maji pamoja na mbinu za kurejesha uhalisia kwenye meneo ambayo yameathiriwa na shughuli za kibinadamu au majanga ya asili” alieleza Dkt. Jangu.

Mkurugenzi wa Tafiti za Mazingira amesema matokeo ya utafiti huo yanatoa muelekeo wa hali ilivyo na kujua kama ni bado ni muelekeo sahihi au kuna maeneo ya kufanyiwa kazi na ndio maana kwenye eneo la utafiti NEMC inafanya kazi na wadau pamoja na taasisi zingine kama ilivyo kwenye mradi huu kati ya SUA, NEMC na wadau wengine.

Mradi huu wa Utafiti unatekelezwa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kwa kushirikiana na Baraza la Taifa la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na kutekelezwa katika bonde la mto Rufiji ndani ya dakio la mto Mbarali kwa ushirikiano na Bodi ya Maji ya mto Rufiji, jumuiya za watumia maji, Wakala wa Huduma za Misitu (TFS), Wilaya ya Mbarali na Wanging`ombe na jamii, kwa ufadhili wa program ya Mazingira ya Umoja wa Mataifa, UNEP, kupitia michango ya nchi kumi wanachama wa Azimio la Nairobi ambapo kwa Tanzania ni kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira, katika kutekeleza Mpango Mkakati wa Kivitendo wa Magharibi mwa Bahari ya Hindi chini ya uratibu wa Sekretarieti ya Azimio la Nairobi.

Mtafiti Mkuu wa Mradi wa EFLOWS kutoka (SUA) Prof. Japhet Kashaigili akieleza malengo ya warsha hiyo.

Mkurugenzi wa Tafiti za Mazingira kutoka (NEMC) Dkt. Menan Jangu akitoa salamu za NEMC.











Dkt. Winfred Mbungu akitoa matokeo ya tathimini ya maji kwa mazingira na mtiririko wake kwenye mto Mbarali.





Post a Comment

0 Comments