SUAMEDIA

Wanafunzi kidato cha tano, sita Zanzibar waaswa kujiandaa kujiunga na SUA

 

Na: Asifiwe Mbembela

Wanafunzi wa kidato cha tano na sita katika Shule ya Sekondari ya Dkt. Salmin Amour Juma iliyopo Chumbuni Mkoa wa Mjini Magharibi, Zanzibar wametakiwa kuchangamkia fursa ya kusoma katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) ili kuweza kutimiza ndoto zao.


Wito huo umetolewa na Mhadhiri wa Lishe na Sayansi ya Mlaji Bi. Zahra Majili wakati akiongea na wanafunzi hao kwenye ziara maalum iliyofanywa na baadhi ya wafanyakazi wa SUA kwenye shule hiyo kwa ajili ya kuwaelezea programu ambazo zinatolewa na Chuo hicho, tukio lililofanyika katika Uwanja wa nje wa Shule hiyo Agosti 02, 2023.

 Bi. Zahra Majili amewaeleza wanafunzi hao kuwa ili waweze kutimiza ndoto zao, wanaweza kujiunga na Chuo cha SUA kwani kimekuwa kikiwaandaa wanafunzi kwa njia ya vitendo ambavyo vinawaruhusu hata baada ya kuhitimu kuweza kujiajiri pamoja na masomo ya nadharia.

 “Wanangu niwaambie tu mko hapa lakini kesho mtakuwa kwenye mahitaji ya kujiunga na elimu ya juu, sasa mkifika hapo naomba mchangue kusoma SUA kwa sababu tuna programu ambazo zitawapa nafasi ya kuwaandaa vizuri, mtaweza kujiajiri ama kuajiriwa,” alisema Bi. Zahra.

 Aidha, Mhadhiri huyo amewaambia wanafunzi hao kuwa programu ambazo zinatolewa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo zinaendana na Sera ya sasa ya Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kuhusu uchumi wa bluu ambapo amebainisha kuwa programu kama Shahada ya Sayansi ya Viumbe Hai na Shahada ya Sayansi ya Mazingira na Usimamizi zina mahusiano ya moja kwa moja na uchumi wa bluu.

Bi. Mawesa Ukani, Afisa Udahili kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo akizungumza katika hadhara ya wanafunzi hao ambao ni mchanganyiko wa masomo ya CBG na PCB amesema kupitia masomo wanayosoma ufaulu unaohitajika ili wawe na sifa za kudahiliwa katika Chuo cha SUA ni ufaulu wa pointi 4 wa daraja DD au CE.

 Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo kupitia baadhi ya wafanyakazi ambao wanashiriki Maonesho ya 4 ya Elimu ya Juu Zanzibar kimeanza ziara ya kutembelea Shule mbalimbali zinazofundisha masomo ya sayansi hapa Visiwani kwa ajili ya kukitambulisha Chuo hicho na kuongeza udahili wa wanafunzi kutoka Zanzibar.



 

Post a Comment

0 Comments