SUAMEDIA

SUA yatoa elimu ya kilimo cha umwagiliaji yenye kuleta tija maeneo ya miinuko

 

Na: Farida mkongwe

Imeelezwa kuwa Elimu ya Kilimo cha Umwagiliaji katika maeneo yenye Miinuko inayotolewa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) iwapo itazingatiwa ipasavyo itakuwa ni njia tosha ya kumuwezesha mkulima wa maeneo hayo kulima na kupata mazao yenye tija pamoja na kutunza mazingira.


Hayo yameelezwa Agosti 6, 2023 na Mhadhiri kutoka Shule Kuu ya Elimu SUA Dkt. Khalifan Hassan Hamidu wakati akizungumza na SUAMEDIA katika banda la SUA kwenye Maonesho ya Wakulima, Wafugaji na Wavuvi Kanda ya Mashariki yanayoendelea katika viwanja vya Mwl. Julius Nyerere mjini Morogoro.

Dkt. Hamidu amesema katika banda hilo wanaonesha namna wanavyowaandaa Maafisa Ugani wanaojifunza kuwa walimu katika sehemu mbalimbali ikiwemo sehemu ambazo zina wakulima kuendesha kilimo cha umwagiliaji bila wakulima kulalamikia uhaba wa maji au mazao kutokuwa  vizuri kwa sababu hakutakuwa tena na changamoto ya ukosefu wa maji.

“Kwa mfano Afisa Ugani anataka kwenda kufundisha au kuelekeza kilimo cha umwagiliaji kwenye maeneo ya miinuko au pembezoni mwa milima, jambo la kwanza atachimba bwawa litakaloweza kutunza maji kwa mwaka mzima ambapo chanzo chake kitakuwa ni mvua au chemichemi, pia atatengeneza mfereji ambao kwa mbele utaunganishwa na vijaruba vitatu, cha kwanza kitakuwa karibu na bwawa, cha pili kitakuwa mbali kidogo na bwawa na cha tatu kitakuwa bondeni kidogo mwa mteremko wa mlima”, amesema Dkt. Hamidu

Amesema baada ya hatua hiyo Afisa Ugani atatengeneza mageti,  geti la kwanza litakuwa na kizuizi cha maji yasiendelee kwenda bondeni kwenye mfereji mkuu lakini kunakuwa na mfereji mdogo unaoingia kwenye kijaruba cha kwanza kwa hiyo ataweka hicho kizuizi cha maji kinachozuia maji yasiende bondeni ila atafungua kile kizuizi cha maji ambacho kinapeleka maji kwenye kijaruba cha kwanza ambacho amepanda aina ya kwanza ya zao kwa sababu anaweza kuwa na vijaruba kama vitatu au vinne akapanda mazao tofauti.

“Kwa hiyo atafungua maji katika kiwango atakachoona yeye kinafaa ili kutunza maji na kuzuia maji yasipotee akimaliza atafunga, atafungua tena kwenye kijaruba kingine mpaka anamaliza, hii inasaidia sana kutunza maji yasipotee pande zote za shamba upande wa bondeni na upande wa mwinuko na kilimo hiki anaweza kukifanya kwa muda wa miaka mitatu”, amesema Mhadhiri huyo.

Amesema Afisa Ugani  anayewaelimisha watu anapaswa awaelimishe kwa vitendo akiwa na zana au kifaa ambacho kinasaidia kuwafanya wakulima au wanafunzi waelewe kwa kuona , kwa kujaribu na kutenda na ndio maana na wao wamekuja na zana hizo katika Maonesho hayo ya Nanenane.

Post a Comment

0 Comments