SUAMEDIA

SUA ya kwanza kutengeneza teknolojia za kisasa zinazoleta tija kwenye kilimo

 

Na: Farida Mkongwe

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimekuwa Chuo cha Kwanza Tanzania kutengeneza teknolojia za kisasa za kilimo ambazo zinapunguza gharama za uzalishaji wa mazao na hivyo kufanya kilimo kiwe chenye tija nchini.



Mkufunzi Msaidizi kutoka Idara ya Uhandisi Kilimo iliyopo Shule ya Uhandisi na Teknolojia SUA Mhandisi Donat Thomas Shukuru akionesha mojawapo ya teknolojia ya kisasa inayotumika kwenye kilimo. Picha na Asifiwe Mbembela.

Kauli hiyo imetolewa Julai 22, 2023 na Mkufunzi Msaidizi kutoka Idara ya Uhandisi Kilimo iliyopo Shule ya Uhandisi na Teknolojia SUA Mhandisi Donat Thomas Shukuru wakati akizungumzia teknolojia mpya zinazolishwa na Chuo hicho katika Maonesho ya Vyuo Vikuu yanayofanyika katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar Es Salaam.

Mhandisi Donat amesema Chuo cha SUA kimejikita katika kufanya tafiti mbalimbali ambazo zinalenga kufanya kilimo kuwa na tija na ndio sababu wamekuja na teknolojia ya roboti inalojiendesha yenyewe inayotumika kwenye uwekaji wa mbolea pamoja na upigaji dawa za kuua magugu na wadudu shambani.

“Hii teknolojia tunasema inaleta tija kwa sababu inamsaidia mkulima aweze kupiga dawa au kuweka mbolea sehemu inayohusika tu yaani sehemu yenye matatizo na hivyo inapunguza gharama za uzalishaji”, amesema Mhandisi Donat.

Teknolojia nyingine ni teknolojia za simu ambazo zimegunduliwa na wanafunzi pamoja na Wasimamizi wa Maabara ya Shule ya Uhandisi na Teknolojia ikiwemo Programu ya Mwagilia ambayo ni ya kwanza kabisa Tanzania inayotumia taarifa kutoka kwenye satellite kutoa ushauri wa kiasi cha maji kinachohitajika kumwagiliwa shambani, na kinatoa makadirio ya kiasi cha maji kinachohitajika kila siku kwa wiki nzima.

Amezitaja Teknolojia nyingine kuwa ni Programu ya kubaini mimea pamoja na matatizo ambayo yapo kwenye mimea hivyo kumsaidia mkulima kutambua matatizo ya mmea na kumpa njia ya kutatua matatizo hayo.

“Tuna Program nyingi, nyingine ni ile ya simu inayoitwa Smart TB ambayo inawasaidia madaktari pamoja na wagonjwa wa TB kwa kuweka kumbukumbu za wagonjwa na kuwakumbusha muda wa kunywa dawa ambapo kwa upande wa madaktari inawasaidia kujua mgonjwa amebakiza muda gani ili arudi hospitali kiasi kwamba akisahau madaktari wanaweza kumuita mgonjwa ili aweze kupata matibabu”, amesema Mhandisi huyo.



 Mhandisi Donat Thomas Shukuru akitoa maelekezo ya matumizi ya teknoliojia za kisasa kwa mwandishi wa habari Farida mkongwe kutoka SUAMEDIA.  
Picha na Asifiwe Mbembela.


Post a Comment

0 Comments