SUAMEDIA

SUA yakabidhi Jukwaa Shirikishi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu

 Na; Gerald Lwomile - Dodoma

Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu imekipongeza Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kwa kuhakikisha kinafanyakazi pamoja na Serikali na kutumia tafiti na rasilimali zake kunufaisha wananchi katika sekta mbalimbali ikiwemo namna ya kujiandaa kukabiliana na majanga.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu, Dkt. Jim Yonazi akizindua Jukwaa Shirikishi la Mawasiliano la Kidijitali la Afya Moja, kulia Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo, Prof. Raphael Chibunda. 

Akizungumza Juni 30, 2023 wakati wa uzinduzi wa Jukwaa Shirikishi la Mawasiliano la Kidigitali la Afya Moja, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu, Dkt. Jim Yonazi amesema SUA ikishirikisha na Ofisi ya Waziri Mkuu Idara ya Menejimenti ya Maafa imekuja na mfumo bora wa utoaji taarifa kidijitali na kurahisisha kukabiliana na majanga yanayoweza kujitokeza.

Dkt. Yonazi amesema vyuo vikuu nchini ikiwemo SUA vinao wajibu mkubwa katika kufanya tafiti kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali ikiwemo vyombo vya ulinzi na usalama kwani kwa kufanya hivyo kama taifa litakuwa na uwezo mkubwa wa kukabiliana na maafa yakiwemo ya moto, magonjwa ya mlipuko na majanga mengine mbalimbali.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu, Dkt. Jim Yonazi akifafanua kuhusu umuhimu wa Afya Moja

“Tumeshaona ongezeko la wananchi, tunaona mabadiliko ya teknolojia je mifumo hii itadumu kwa muda gani? au kuna mifumo mingine tunaweza kuitafuta au kuitengeneza ikatusaidia katika kituo chetu, huenda kituo hiki kikazaa vituo vingine, changamoto hii niitoe kwenu nyinyi wataalamu lakini pia kwa vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama” amesema Dkt. Yonazi

Awali akikabidhi Mradi huo wa Jukwaa Shirikishi la Mawasiliano la Kidijitali la Afya Moja, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo, Prof. Raphael Chibunda amesema uwepo wa Jukwaa hilo utaimarisha uwezo wa nchi katika kubaini uwepo wa viashiria vya majanga yanayoweza kudhuru afya ya binadamu ikiwemo magonjwa ya mlipuko na matukio mengine na kuyatolea taarifa kwa wadau.

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo, Prof. Raphael Chibunda (aliyesimama) akitoa maelezo ya utekelezaji wa Jukwaa hilo, aliyekaa ni Dkt. Jim Yonazi

“Katika kuhakikisha Jukwaa hili linafanya kazi kama lilivyokusudiwa, Chuo chetu kilitoa vifaa vya tehema ili kufanikisha huu mradi, vifaa hivyo vina thamani ya shilingi milioni 42.3 kwenye hivyo vifaa kuna seva 1, kifaa cha huduma kwa wateja na komputa 8” amesema Prof. Chibunda.

Akitoa taarifa ya mradi huo Afisa Tehema Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Bw. Alex Ndimbo amesema endapo jukwaa hilo litatumika kikamilifu litaimirisha sehemu ya Afya Moja na wizara za kisekta katika uwezo wao wa kutambua matukio ya ugonjwa pamoja na ishara na taarifa za awali zinazohusiana na chanzo cha ugonjwa au tukio lolote kijografia au kijiorojia na kuchakata takwimu hizo mapema ili kutoa tahadhari ya mapema katika kuratibu kabla ya kutokea mlipuko mkubwa wa ugonjwa au madhara yoyote kwa jamii.

Amesema kupitia jukwaa hili wananchi wataweza kutoa taarifa mbalimbali za maafa kwa njia ya kupiga simu, ujumbe mfupi na hata ‘WhatsApp’ na hivyo kurahisisha namna ya kukabiliana na majanga.

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo kupitia Mradi wa ‘Sacids Foundation’ kimeshirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu katika kuhakikisha Jukwaa hilo Shirikishi la Mawasiliano la Kidigitali la Afya Moja kwa kutoa vifaa, kiteknolojia na ufundi.







                      Picha juu ni wadau mbalimbali katika uzinduzi wa Jukwaa hilo

 

Post a Comment

0 Comments