SUAMEDIA

SUA watakiwa kuendelea kumuenzi Hayati Sokoine kwa vitendo

Na: Winfrida Nicolaus

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo  kama kilivyopewa dhamana ya kutunza jina la Hayati Edward Moringe Sokoine ikiwa ni alama ya kudumu ya kiongozi huyo shupavu na mahiri kimetakiwa kuendeleza jitihada za kukuza Sekta ya Kilimo nchini kwa kuendelea kufanya Tafiti kwa nguvu zote na kutoa mafunzo stahiki kama sehemu ya kuenzi mchango wa Sokoine.

Mkuu wa Wilaya ya Mvomero Mhe. Judith Ngulu akizungumza kwenye Mdahalo wa kumbukizi ya Hayati Sokoine.

 Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Mvomero Mhe. Judith Ngulu ambaye alikuwa mgeni rasmi katika Mdahalo wa Kitaifa wa Maadhimisho ya Kumbukizi ya 18 ya Hayati Edward Moringe Sokoine na hitimisho la Maadhimisho hayo  ambayo yaliyoanza Mei 23, 2023 katika Kampasi Kuu ya Edward Moringe Mkoani Morogoro.

Amesema wanapokutana katika Kumbukizi ya Hayati Edward Moringe wasiishie tu kusherehekea maisha yake ya kuvutia bali waweke nadhiri ya kuendeleza maono yake na kuiga matendo mazuri ikiwa ni pamoja na namna alivyojitoa kuwatumikia watanzania na kuwaletea maendeleo kwa kipindi cha uhai wake kwakuwa alihimiza kwa kiasi kikubwa mabadiliko katika nyanja mbalimbali ikiwemo kilimo, mifugo, elimu, viwanda pamoja na sekta zingine.

Aidha amesema anatambua kuwa uanzishwaji wa (SUA) ni sehemu ya matunda ya Hayati Sokoine na maono yake pia na matokeo ya utendaji kazi wake yanaonekana hivyo (SUA) inatambulika kama Chuo mama ambacho kimekuwa kikitoa mchango mkubwa kwa Serikali na hata Taifa katika maswala ya tafiti, kutoa mafunzo, ubunifu wa vitu mbalimbali kwani hayo ni matokeo ya matunda ambayo Hayati Sokoine ameyaacha.

“Hayati Sokoine alisisitiza kujitosheleza kwa chakula, ninamnukuu alisema “Wajibu wa kila Mtanzania kila familia na anayekula na kujilisha yeye mwenyewe si wajibu wa Taifa kumlisha mtu, unaweza ukasaidiwa unapopatikana na janga lakini kama hauna janga ni wajibu wa kila mtu aweze kujitosheleza kwa chakula na atoe ziada kwa Taifa kauli hii aliitoa octoba 4, 1983”, alisema Mhek Nguli

Mhe. Judith ameongeza kwa kuwaambia vijana kuwa wamepewa fursa na Serikali imeweka nguvu kubwa kwao hivyo wanatakiwa kuachana na ujana ambao umepitiliza utakaowasababisha kushindwa kutimiza malengo yao na kukumbuka kuwa kuna maisha baada ya ujana.

Kwa upande wake Makamu wa Mkuu wa Chuo Kikuu Cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda amesema wanafanya mihadhara ya Kumbukizi ya Sokoine aliyekuwa Waziri Mkuu wa Tanzania kwa vipindi viwili tofauti mwaka 1977 – 1980 na 1983 – 1984 kutokana na ushiriki wake mkubwa katika harakati za kuanzishwa kwa Chuo hicho vilevile kutambua mchango wake katika maendeleo ya nchi.

Makamu wa Mkuu wa Chuo Kikuu Cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda akieleza malengo ya SUA kufanya kumbukizi hiyo.

Amesema tangu kuanzishwa kwa kumbukizi hizo mada mbalimbali kuhusiana na maswala kama vile mfumo wa Vyama vingi, Demokrasia, Rushwa, Kupambana na Umasikini, Tanzania baada ya Nyerere, Usalama wa Chakula, Maendeleo ya Kilimo, Elimu, Utafiti, Utatuzi wa Migogoro, Utandawazi na mambo mengine yanayohusiana na maswala ya Kijamii, Kisiasa na Kiuchumi yamejadiliwa.

Prof. Chibunda ameongeza kuwa Kauli Mbiu ya mwaka huu inalenga kuhamasisha vijana kushiriki kikamilifu katika Sekta ya ilimo, ufugaji na uvuvi kwa kuweka Mazingira rafiki, Sera na Miongozo inayowawezesha kufanya shughuli za kilimo, ufugaji na Uvuvi kwa ufanisi.

‘‘Kauli mbiu hii inaumuhimu mkubwa katika kuendeleza kazi na ndoto za Hayati Edward Moringe Sokoine na kuwapa vijana matumaini na muongozo wa kufanikiwa katika Sekta hizi muhimu”, amesisitiza Prof. Chibunda.

Wageni mbalimbali wakifuatilia mdahalo huo wa 18 wa kumbukizi ya Hayati Sokoine uliofanyika katika Kampasi ya Edward Moringe Mkoani Morogoro.



Post a Comment

0 Comments