SUAMEDIA

WANAFUNZI SUA WAISHUKURU SERIKALI KWA MSAADA WA VISHIKWAMBI

 Na: Adam Maruma.

Kaimu Mshauri wa Wanafunzi Chuo Kikuu cha Sokoine Cha Kilimo SUA, Bi Hilda Gamuya, ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwapatia msaada wa Vishikwambi (Tablet) wanafunzi wenye uhitaji maalum wanaosoma mwaka wa kwanza katika Kozi mbalimbali chuoni hapo ili viwasaidie kujifunza masomo yao kwa urahisi na kuendana na Kasi ya wenzao darasani.

Baadhi ya wanafunzi hao walionufaika na msaada wa Vishikwambi wakiwa kwenye picha ya pamoja.
Bi. Hilda amesema hayo Ofisini kwake wakati akigawa vifaa hivyo   ambavyo ni Vishikwambi 25, na kuongeza kuwa vimekuja muda muafaka kutokana na wanafunzi wenye uhitaji Maalum hasa wenye changamoto ya usikivu Hafifu kuongezeka kwa siku za hivi karibuni chuoni hapo,   huku idadi kwa sasa ikiwa ni takribani wanafunzi 33 ambao wamejitokeza na kukubali kusaidiwa na wameanza kuwasaidia wale walioathirika Zaidi na changamoto hiyo.

Amesema kwa msaada huo ambao Serikali imetoa ni jambo la kupongezwa, kwani kifaa hicho pamoja na kutumika kutunzia kumbukumbu ya kinachofundishwa darasani pia wanafunzi hao watakua na uwezo wa Kuongeza maarifa katika kusaka machapisho mengine kwenye mitandao mingine ya kitaaluma kwa kile ambacho mwalimu atakua amekiwalisha kwa siku husika.

Bi. Hilda Gamuya amesema msaada huo haukuishia tu kwenye Vishikwambi kwani pia Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, imewapatia wanafunzi hao wenye changamoto mbalimbali Bajaji 2 ambazo moja itakuwa Kampasi Kuu ya Edward Moringe na nyingine itakua Kampasi ya Solomon Mahlangu, na zitatumika kwa usafiri kwa kundi hilo maalum ili na wao wajione ni watu  Muhimu katika nchi yao na  jamii inufaike kwa maarifa ambayo SUA itawapatia kwa kipindi chote cha Masomo yao hapo Chuoni.

Mmoja wa Wanufaika wa msaada huo Zuhura Ally ambae ni  mwanafunzi wa mwaka wa pili wa Shahada ya Ualimu chuoni hapo,  akitoa neno la shukrani kwa niaba ya wenzake huku akiongea kwa hisia kali amesema wao kama wanufaika wa msaada huo, hawana cha kuilipa Serikali yao pendwa Zaidi ya kumtakia Afya njema Rais Mh. Samia Suluhu Hassani ili aendelee kuwaona wao kama kundi linalohitaji uangalizi wa karibu Zaidi kwa kuwa safari yao ya kusaka elimu ina mengi ya kukatisha tamaa.

“Kuna kipindi niliwaza kuacha masomo yangu hapa SUA, kwa sababu kila mwalimu akiingia darasani kufundisha nakuwa na changamoto kuona hata nikikaa mbele nakuwa napishana na  kile anachofundisha mwalimu hadi anamaliza kipindi chote sielewi zaidi  naona kama napoteza muda wangu darasani, kwa kweli ilinikatisha tamaa nakuona ndoto yangu ya kuhitimu Shahada yangu inakufa kwasababu naona safari yangu ya kimasomo hapa SUA, inafikia mwisho wake, Lakini kwa vifaa hivi naanza kuona matumaini tena kwa kweli nawashukuru sana na namtakia Afya njema Rais Samia Suluhu Hassan, kwa vifaa hivi”, amesema  Zuhura .

 Nae Dkt. Thabitha Lupeja ambae ni Mkuu wa Idara ya Mitaala na Ufundishaji  kutoka Shule Kuu ya Elimu, SUA, ambae pia ni Mratibu wa Mahitaji Maalum  amesema Mradi huo wa kugawa vifaa kwa Wanafunzi hao ulianza mwaka jana baada ya kuwapima wanafunzi uwezo wa usikivu na baada ya majibu wapo waliotakiwa kupatiwa matibabu ili kurudisha usikivu wao, na wengine ikaonekana wapatiwe vifaa kama hivyo na amefurahishwa na msaada wa vifaa hivyo kwani itakuwa ni chachu kwa wanafunzi hao kufanya vizuri katika masomo yao maana bila msaada huo ni wazi wanafunzi hao hali zao kitaaluma zingekua ngumu sana.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Serikali ya wanafunzi SUASO, katika zoezi la ugawaji wa Vifaa hivyo Peter John ambae ni Naibu Waziri wa Asasi Jinsia na Watu Wenye Mahitaji Maalum amesema Serikali ya wanafunzi ya imeipongeza Serikali na SUA kwa ujumla kwa kuwajali wanafunzi wenzao wenye Changamoto mbalimbali kwani na wao ni Binadamu na wanahitaji kuungwa mkono kwa kufikia ngazi ya juu ya kutafuta elimu ya Chuo Kikuu.

PICHA MBALIMBALI ZIKIONESHA WANAFUNZI HAO WAKIKABIDHIWA VISHIKWAMBI.






 


Post a Comment

0 Comments