SUAMEDIA

SUA kuhakikisha Afya ya Mlaji na Mkulima inalindwa

Na Amina Hezron,Morogoro

Katika kuhakikisha Afya ya Mlaji na Mkulima inalindwa  Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia Idara ya Mimea Vipando na Kilimo cha Bustani imetoa mafunzo kwa wakulima kuhusiana na matumizi ya mbinu za Kilimo Ikolojia katika uzalishaji ambazo zitawasaidi kuepukana na matumizi ya pembejeo za viwandani kwa kiasi kikubwa.

Akizungumza katika Mafunzo hayo Mhadhiri kutoka SUA Dkt. Ramadhani Majubwa amesema kuwa kilimo ikolojia kinalenga hasa kuhakikisha mkulima anatumia mbinu rafiki ambazo zinatunza mazingira pamoja na kutunza viumbe hai ambao wanapatikana katika eneo husika.

“Tumelenga kuwafundisha wakulima kuzalisha mazao ambayo hayatakuwa na sumu pamoja na kuwapunguzia athari zinazoweza kutokea kutokana na upuliziaji wa dawa shambani ambazo mara nyingi dawa hizo huweza kuwarudia wenyewe na kuweza kusababisha athari za kiafya”, alisema Dkt. Majubwa.

Aidha amewataka wakulima kuacha  kilimo cha mazoea na badala yake  kuingia katika kilimo cha kiikolojia kwa kuwa njia hiyo itawasaidia kukabiliana na mabadiliko ya tabia ya nchi yanaendelea kutokea duniani lakini pia kupunguza gharama za matumizi ya pesa kwa ajili manunuzi ya pembejeo huku ikiongeza uzalisahaji wa mazao kutokana na ongezeko la wadudu rafiki kama vile nyuki ambao wanasaidia katika uchavushaji. 

Kwa upande wake Mkulima kutoka katika Kijiji cha Ruvuma Kata ya Mlimani mkoani Morogoro Bi Chagua Kibwana ameipongeza SUA kwa mafunzo hayo na amewataka wakulima wengine kulima kilimo hicho ili kuepukana na gharama zisizo na msingi za ununuaji wa mbolea na badala yake utatumia mbolea za asili.

“Hapa nimeona mazao yaliyotumia mbolea za asili yamenoga ukilinganisha na yale ambayo hayajatumia kabisa pamoja na yale yaliyotumia pembejeo za viwandani kwa kweli nilikuwa sijui kama kuna umuhimu wa kuwa na boksi la usafi shambani wala kama kuna wadudu rafiki shambani, alisema Bi. Kibwana.

Naye Mkulima mwingine Bw. Geukeni Asifiwe amesema kuwa mafunzo hayo yamemsaidia kufahamu faida za kilimo hai ambacho mojawapo ya mambo muhimu ni kutunza wadudu rafiki ambao husaidia kuua wadudu shambani badala ya kutumia viuatilifu ambayo vinaathari hadi kwa walaji.

Mafunzo hayo ya siku tatu yameanza na  wakulima wa Kijiji cha Ruvuma Kata ya Mlimani na  Sept 13 watashiriki wakulima wa Kinyenze Vitonga na Mlali  kabla ya wakulima wa Kiroka kutoka Morogoro Vijijini.

 


Post a Comment

0 Comments