Na: Sharon Sauwa
Dodoma.
Ofisi ya Taifa ya Takwimu Tanzania (NBS) imesema watu
waliohesabiwa wamefikia asilimia 99.93 na waliobakia ni asilimia 0.07 ya kaya
zote nchini hadi kufikia leo asubuhi.
Akizungumza leo Jumatano, Agosti 31, 2022 Mtakwimu Mkuu wa
Serikali, Dk Albina Chuwa amesema asilimia 0.07 ya kaya zilizobakia zitandelea
kuhesabiwa hadi Septemba 5, 2022.
“Simu zilizotolewa zitatumika kuwafikia ambao hawajahesabiwa
kwa kuwa utaratibu maalum ulishaandaliwa namna ya kuzifikia kaya hizo kupitia
viongozi wa mitaa na vitongoji,”alisema.
Kwa upande wa sensa ya majengo, Dk Chuwa alisema hadi leo
asubuhi jumla ya majengo 6,351,927 yalikuwa yameshahesabiwa ambapo taarifa za
umiliki, mahali yalipo na taarifa nyingine zilizoainishwa katika dodoso la
majengo zimekusanywa.
Amesema makadirio ya operesheni anwani za makazi wanategemea
kufikia majengo milioni 12.7 kwa nchi nzima.
“Bajeti iliyoidhinishwa na Bunge kwa mwaka wa fedha 2022/2023
ni Sh400 bilioni sawa na wastani wa Sh6, 265 au Dola za Marekani 2.7 kwa mtu
mmoja,” amesema Dk Chuwa.
Amesema misaada kutoka kwa wadau wa nje ya nchi ilikuwa ni
kuwajengea uwezo wataalam na vishikwambi.
Amefafanua kuwa msaada wa kuwajengea uwezo wataalam ulitolewa
na nchi ya Marekani wakati vishikwambi vilitolewa na Korea Kusini, Shirika la Kimataifa
la Kuhudumia Watoto (Unicef) na Shirika la Umoja wa Mataifa la Wanawake (UN
Women).
Aidha, amesema mkataba wa ajira za muda kwa ajili ya kazi za
sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 baina ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu na
makarani au wasimamizi wa sensa ambao ulianza Agosti 21, 2022 hadi Septemba
Mosi, 2022 haujabadilika.
“Kuanzia Septemba 2 hadi 5, 2022 iwapo kuna mtu ambaye atakuwa
hajahesabiwa au majengo ambayo yatakuwa hayajahesabiwa. Mwananchi au mtu huyo
anatakiwa kuwasiliana na viongozi wake wa Serikali na mitaa au kitongoji au
kupiga simu kwa namba ambazo zimetolewa ili utaratibu wa kukusanya taarifa
ufanyike,” amesema Dk Chuwa.
0 Comments