NA:Winfrida Nicolaus
Taasisi ya Kuwajengea Uwezo Wajasiriamali katika harakati zao za kujiletea Maendeleo (AICAD) imeendelea na kazi yake ya kuwajengea uwezo Wajasiriamali pamoja na Wakulima kwa kutumia Teknolojia zinazozalishwa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA ili kuwawezesha wakulima hao kujikwamua na hali duni ya kimaisha.
Amebainisha hayo Afisa Programu
wa AICAD Bw. Florence Rugimbana Agosti 06, 2022 wakati akizungumza mubashara
kupitia SUA Radio kutoka kwenye viwanja vya Maonesho ya 29 ya Wakulima,
Wafugaji na Wavuvi Kanda ya Mashariki yanayofanyika Mkoani Morogoro.
Amesema Taasisi ya Kuwajengea
Uwezo Wajasiriamali (AICAD) inafanya kazi zake kwa kushirikiana na Vyuo Vikuu
Pamoja na Taasisi zingine zinazozalisha Teknolojia mbalimbali ambapo kazi yake
haswa ni kuweka daraja kati ya wazalishaji Teknolojia ambao ni vyuo vikuu
ikiwemo SUA.
Bw. Rugimbana amesema lengo la
kufanya mashirikiano na SUA ni kutumia Teknolojia ambazo wanazizalisha hasa
katika Kilimo kuwajengea uwezo wajasiriamali kwa kuwapatia mafuzo na wao
kuyatumia ili kujikwamua kiuchumi.
Aidha amesema Taasisi ya AICAD
pia inafanya Tafiti mbalimbali kwenye jamii kuona wanakabiliana na changamoto
gani au wanarasilimali zipi ambapo baada ya kuzitambua wanarudi kwenye taasisi
ambazo zinazalisha Teknolojia ili kupata majibu ya namna ya kutatua changamoto
hizo ikiwemo kwa Wakulima, Wafugaji pamoja na Wajasiliamali kwa ujumla.
“Tumekuja kwenye Maonesho haya
ya 29 hapa kwenye banda la SUA ili kuwaeleza wananchi AICAD ni nini, kuonesha
baadhi ya bidhaa kutoka kwa wajasiriamali ambao wamefuzu kozi zetu mbalimbali
ambazo tunazitoa ikiwemo Usindikaji na Uongezaji wa thamani wa Mazao ya Kilimo,
Uongezaji na Uboreshaji wa Kazi za Mikono vyote hivyo vimetolewa na AICAD”,
amesema Bw. Rugimbana.
Ameongeza kuwa AICAD inatoa
Mafunzo mbalimbali ya siku 10 hadi 15 pia wana machapisho kutoka kwenye tafiti
mbalimbali ambazo wamezifanya pamoja na vitini kwaajili ya Mafunzo zaidi.





0 Comments