SUAMEDIA

Wanawake na Wanafunzi SUA watakiwa kuripoti vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia

 

Na: Gladness Mphuru

Mkuu wa Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro Mhe. Halima Okash amewataka wanawake wabadili fikra potofu na kujenga fikra chanya, ili waweze kushiriki kikamilifu kuleta maendeleo endelevu na kujenga taifa lenye usawa katika nyanja zote kisiasa, kiuchumi, kijamii na kitamaduni.

 Mhe. Okash ameyasema hayo katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani March 8, 2022 wilayani Mvomero mkoani Morogoro, akiambatana na Katibu wa UWT Wilaya ya Mvomero, Afisa Mipango Wilaya ya Mvomero akimuwakilisha Mkurugenzi wa Halmashauri pamoja na Taasisi mbalimbali ikiwemo Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA.

 “Naomba nitoe rai kwa wanawake wenzangu kubadili fikra na mitazamo kwa kujiona kwamba wao ni watu ambao hawawezi kufanya maamuzi, sisi wanawake na wanaume tupo tofauti kwenye maumbile lakini kwenye masuala ya uwezo wa kiutendaji wanawake wanaweza kushiriki kikamilifu katika kujenga Taifa lenye maendeleo makubwa”

 Mhe. Okash amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa sh. Bilion 3.25 kupitia mpango wa maendeleo ya Taifa na mapambano dhidi ya UVIKO 19, ambazo zimetumika katika Sekta ya Afya pamoja na ujenzi wa madarasa 122 kwa shule za sekondari na msingi wilayani humo.

 Akizungumza mara baada ya kutoka kwenye Maadhimisho yaliyofanyika wilayani Mvomero, katika ukumbi wa SUA nanenane Manispaa ya Morogoro Mratibu wa masuala ya Jinsia kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Dkt. Charles Lyimo, kwenye hafla fupi iliyoandaliwa na Chama cha Wafanyakazi cha (RAAWU), amewaasa wanawake wa SUA wafanyakazi na wanafunzi kutumia Vyama vya kijinsia, Kamati ya Kudhibiti Uadilifu (KKU) na Serikali ya Wanafunzi SUA (SUASO) kuwasilisha malalamiko yao, ili kupunguza unyanyasaji wa kijinsia katika maeneo kazi na masomoni ili kufikia usawa wa kijinsia.

“Napenda kuwasihi wafanyakazi pamoja na wanafunzi tutumie vyombo vyetu hivi ambavyo vipo chini ya uongozi wa Chuo ili tuweze kujiamini katika kusoma na kufanya kazi katika mazingira ambayo ni salama, kwahiyo napenda pia kutumia Maadhimisho haya ya Wanawake Duniani tuweze kuonesha taswira kuwa SUA ni moja ya Taasisi ambayo imeweka mazingira bora ya kazi pamoja na masomo”.



















Post a Comment

0 Comments