SUAMEDIA

Ofisi Ya Rais-Utumishi yadhamiria kuwa ya kwanza kukamilisha Ujenzi wa Ofisi za kudumu katika Mji wa Serikali ili kutoa huduma bora kwa Wananchi

 Na. Veronica Mwafisi-Dodoma

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama amekagua maendeleo ya ujenzi wa ofisi za kudumu za Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora unaoendelea katika Mji wa Serikali-Mtumba na kuridhishwa na hatua iliyofikiwa.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na Mkandarasi ambaye ni Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) na Mshauri Elekezi Watumishi Housing (WHC) wanaojenga jengo la ofisi za kudumu za Ofisi ya Rais - UTUMISHI alipoenda kukagua maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo kwenye Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma. Wa kwanza kulia ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Dkt. Laurean Ndumbaro.

Mhe. Jenista ameridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa ofisi hiyo mara baada ya kufanya ukaguzi na kuielekeza Menejimenti ya ofisi yake kuhakikisha inasimamia kikamilifu ili ofisi yake iwe ya kwanza kukamilisha ujenzi na kutoa huduma bora kwa wananchi.

Mhe. Jenista amesema, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ilipata bahati ya kuwekwa kwa jiwe la uzinduzi wa ujenzi wa ofisi za wizara zote katika Mji wa Serikali, hivyo ni vema kuilinda heshima hiyo kwa kuwa wa kwanza kukamilisha ujenzi wa ofisi hizo.

“Nimeridhishwa na maendeleo ya ujenzi kwani kazi inaonekana kuwa ni bora na hata taarifa ya Mshauri Elekezi inaeleza kuwa viwango vya ujenzi vina ubora unaokubalika na unaoendana na thamani ya fedha inayotolewa na Serikali.” Mhe. Jenista ameongeza.

Mhe. Jenista amempongeza Mkandarasi, Mshauri Elekezi na Menejimenti ya ofisi yake kwa kuendelea kusimamia vizuri ujenzi wa ofisi hizo.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro ameungana na Mhe. Jenista Mhagama kumpongeza Mkandarasi ambaye ni Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) na Mshauri Elekezi Watumishi Housing kwa kazi nzuri waliyoifanya ambayo imefikia hatua inayoridhisha.

Dkt. Ndumbaro amewataka TBA na Watumishi Housing kuendelea na kasi hiyo ya ujenzi ili kutekeleza maelekezo ya Mhe. Waziri ya kutaka ofisi yake kuwa ya kwanza kukamilisha ujenzi pamoja na azma ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kutaka wizara zote kukamilisha ujenzi wa ofisi zake katika Mji wa Serikali Mtumba.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akikagua miundombinu ya jengo la ofisi za kudumu za Ofisi ya Rais - UTUMISHI linaloendelea kujengwa na Mkandarasi ambaye ni Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) na Mshauri Elekezi Watumishi Housing katika Mji wa Serikali Mtumba wakati Waziri huyo alipotembelea kuona maendeleo ya ujenzi huo jijini Dodoma.
Muonekano wa Jengo kubwa la kudumu la Ofisi ya Rais - UTUMISHI linaloendelea kujengwa na Mkandarasi ambaye ni Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) na Mshauri Elekezi Watumishi Housing (WHC) wanaojenga Jengo hilo wakati Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama alipotembelea kuona maendeleo ya ujenzi huo kwenye Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akielekea kukagua jengo la ofisi za kudumu za Ofisi ya Rais - UTUMISHI linaloendelea kujengwa katika Mji wa Serikali Mtumba wakati Waziri huyo alipotembelea kuona maendeleo ya ujenzi huo jijini Dodoma. Wapili kutoka kushoto ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa aliweka jiwe la uzinduzi wa ujenzi wa ofisi za wizara zote awamu ya pili katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma tarehe 2 Desemba, 2021 kwenye eneo linalojengwa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma.

Post a Comment

0 Comments