SUAMEDIA

SUA yatoa mafunzo kwa Waganga wa Tiba Asili ili kubadilisha mtazamo na tabia

 

Na: Calvin Edward Gwabara

Morogoro.  

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia mradi wa VaSPHARD kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali wamefanya  mafunzo kwa Waganga wa tiba asili na kisha kupima dawa zao ili waweze kubadilisha mtazamo na tabia  katika kuzalisha dawa ili watengeneze dawa salama,safi na zenye viwango vya juu na kupata usajili.

Mkuu wa Mradi wa VASPHARD Dkt. Faith Mabiki akizungumza kwenye mafunzo hayo ya siku moja ya watengenzaji wa dawa za asili kutoka Mikoa mbalimbali.

Akizungumza na SUAMEDIA Mkuu wa Mradi wa VaSPHARD Dkt. Faith Mabiki amesema kuwa mafunzo hayo yanawakutanisha waganga wa tiba asili na watengenezaji wa dawa zaidi ya 35 kutoka katika mikoa mbalimbali ya Tanzania ambao wamekuja na dawa zao zaidi ya 100 ambazo baada ya majadiliano na kujengeana uelewa wa zoezi hilo zitapimwa na kisha kupewa majibu kujua ubora wa dawa hizo na kuwashauri namna bora za kuzalisha na kufungasha dawa zao kukidhi viwango vya kimataifa.

“Kwahiyo sasa hivi tunajadiliana nao baada ya kuwajengea uelewa na tunaingia nao makubaliano kisha tutakwenda maabara kufanya vipimo viwili ambavyo vimewekwa na serikali ili waweze kutengeneza dawa kiusalama zaidi”. Alieleza Dkt. Mabiki.

Ameongeza “Ili Serikali iweze kuzitangaza dawa hizo lazima wapelekwe kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kuangaliwa vipimo kadhaa kama vile sumu kuvu,vipomo vya wadudu wanaosababisha magonjwa au dawa kuwa chafu, vipimo vya madini tembo  na kemikali iliyo ndani ya dawa hizo, na kwa bahati nzuri vipimo hivyo vyote SUA tunaweza kuvifanya ndio maana Mkemia Mkuu wa Serikali ametupa kufanya baada ya kupata hela kutoka kwa Jumuiya ya Wanataaluma wa Sayansi Afrika tunakwenda kufanya kazi hii”.

Amesema kama kweli Taifa linataka kuona Dawa wanazotengeneza zinachangia afya ya Jamii na maisha ya wataalamu hao wa tiba asili lazima swala la ubora wa dawa hizo lizingatiwe hapo ndipo wataweza kulifikia soko kubwa la ndani ya Tanzania na nje kama ambavyo nchi zingine maarufu kwa uzalishaji wa dawa hizo wamefikia mfano India na China.

Dkt. Mabiki amesema kuwa zoezi la upimaji wa dawa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali lina gharama kubwa kama ambavyo waganga hao wamesema lakini SUA kama taasisi ya Elimu na Utafiti wanavyo vifaa vya kisasa na bora lakini pia wanao wanafunzi wanaofanya tafiti hizo kwenye shahada mbalimbali za Juu ambao wanatumia dawa hizo kuzifanyia utafiti na kupata shahada zao lakini pia waganga wenyewe wenye hizo dawa wanapimiwa dawa zao bure na kupewa ushauri wa namna ya kufanya

Kwa upande wake Mtaalamu wa tiba asili kutoka Njombe Bw. Flavian Nyakeji amesema amefurahi kupata nafasi hiyo ya kipekee ya kuelimishwa na kujua namna ya kutengeneza dawa zenye ubora

“SUA imetusaidia kwa muda mrefu kuboresha utengenezaji wa dawa zetu wanataka tufikie viwango vya juu, na sisi hili ndilo tunalolitaka maana sisi tunaotoka Njombe tunauza Njombe tuu, likini sasa lini tutauza Dar es Salaam, Mwanza, Kenya na lini tutauza Ulaya” amesema Nyakeji.

Nyakeji amesema ameleta dawa kumi kwenye zoezi hilo ili aweze kujua nini kipo kwenye dawa zake hasa kwa kujua ubora wake na yupo tayari kupata ushauri wa kitaalamu wa namna ya kuboresha dawa hizo ili ziweze kuwa na viwango badala ya kuzalisha bila viwango hali ambayo itatunyima usajili na kutofikia soko la nje.

Mtaalamu huyo wa Tiba asili amesema kupitia mafunzo na uwezeshwaji huo wa kitaalamu tayari kuna mabadiliko makubwa kati uzalishaji wa tiba asili nchini na anaamini kuwa kutafanyika mapinduzi makubwa katika soko la tiba asili nchini na wataweza kuuza bidhaa zao nchi ya nchi kama ambavyo nchi zingine zinauza Tanzania.

 Mhadhiri wa kutoka Idara ya Sayansi ya mazao ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Dkt. Richard Madege akiwasilisha mada yake mbele ya waganga hao wa tiba asili





 Washiriki wa mafunzo hayo wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya kumaliza mafunzo hayo.


Post a Comment

0 Comments