SUAMEDIA

Bilioni moja kutekeleza Miradi mitatu ya maji majimbo matatu Wilayani Morogoro

Na.Vedasto George.

Serikali kupitia Wakala wa Maji na Usafi  wa Mazingira  Vijijini RUWASA imeanza kutekeleza Miradi mitatu ya maji kwenye majimbo matatu ya Wilaya ya  Morogoro ambapo hadi kukamilika kwake itagharimu  zaidi ya shilingi Bilioni moja, Miradi ambayo inatajwa  kuondoa  tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi.

Hayo yamebainishwa  na Mhandisi  Grace Lyimo Meneja wa RUWASA   wakati akizungumza na SUAMEDIA ofisini kwake juu ya umuhimu wa Maadhimisho ya Wiki ya Maji  ambayo kilele chake ni Machi 22 kila mwaka.

Mhandisi Lyimo amesema kwa kutambua umuhimu wa rasilimali hiyo  pamoja na changamoto wanazozipata wananchi ikiwemo ya  kutembea umbali mrefu wakitafuta huduma hiyo muhimu ya  maji tayari serikali kupita Mradi wa UVICO 19  imeidhinisha zaidi ya shilingi bilioni moja  fedha ambayo itatumika  kuboresha na kujenga miundombinu   mipya  ya maji.

Mhandisi  huyo  ameitaja miradi hiyo kuwa ni Mradi wa Maji Mvuha ambao utahudumia vijiji  vyote vya maeneo hayo, Mradi wa maji  Kikundi ambao upo Morogoro Kusini Mashariki ambapo ujenzi wa  kisima na tenki lenye ukubwa wa lita 150,000 unaendelea huku mradi mwingine ukiwa ni Mradi wa maji Kauzeni ambao unafanyiwa maboresho.

“Sisi RUWASA wilaya ya Morogoro tumepatiwa  Miradi mitatu kwenye majimbo matatu ya wilaya ya Morogoro  na Mradi mmoja upo jimbo la Morogoro Kusini ambao ni Mradi wa maji Mvuha pale tunaenda kuboresha huduma ya maji kutoa maji kwenye mto Mvuha kuyaingiza kwenye matenki na kuyasambaza kwenye vijiji vyote vya mvua lakini pia tuna miradi ya maji kwenye jimbo la Morogoro Kusini Mashariki pamoja na Mradi wa maji  kwenye jimbo la Morogoro  mjini   pale Kauzeni  na miradi yote hii hadi kukamilika  kwake itatughalimu kiasi cha shilingi bilioni 1.6”,  amesema Mhandisi Lyimo. 

Aidha Mhandisi   huyo amesema  hali ya upatikanaji wa huduma ya  maji safi na salama  katika Halmashauri ya wilaya ya Morogoro  inazidi kuimarika ambapo mpaka sasa watumiaji wa maji zaidi ya 260,000 tayari wamefikiwa  ikiwa ni sawa na 69% ya wakazi wote  huku akisema hadi kufikia mwaka 2025  serikali itakuwa imefikia vijiji vyote katika wilaya hiyo ambavyo bado havijafikiwa na huduma ya maji.

Katika hatua nyingine Mhandisi  Grace Lyimo amesema lengo la kuadhimisha wiki ya maji kila mwaka ni kuikumbusha jamii pamoja na wadau wa maji duniani kote  kuendelea kulinda  na kutunza  vyanzo vya maji huku akisema  Wakala wa Maji na Usafi  wa Mazingira  vijijini RUWASA imeadhimisha wiki ya maji tangu tarehe 16 mwezi huu wa tatu  kwa kupanda miti kwenye vyanzo vya maji zaidi ya 200 huku kwenye kilele cha wiki ya maji wakiwa wamepanda miti 400 kwenye chanzo cha maji cha Mto Mbezi uliopo  kwenye kijiji cha Tegetero  Morogoro vijijini.

Nao baadhi ya wananchi akiwemo AIi  Kapugwa na Mawazo Kaboge kwa pamoja wameishukuru serikali kwa kuanza kutekeleza miradi ya  maji kwenye maeneo  yao huku wakisema ujio wa miradi hiyo pia umesaidia kuwapatia ajira  wao kama vijana wazawa wa vijiji hivyo.

Kwa upande wake Mhandisi Juma Mgaigwa anayeshughulikia Mipango na  Usanifu  wa Miradi RUWASA amesema miradi yote ya maji  inayotekelezwa katika wilaya ya Morogoro kupitia Mradi wa UVICO 19 inatarajiwa kukamilika  ndani ya miezi sita huku Mhandisi JOSEPH PETRO msimamizi wa Mradi wa maji Kikundi kupitia kampuni ya Clalon Technology Company  amewatoa wasiwasi wakazi wa kijiji cha Kikundi na kusema  Mradi huo utakamilika kwa wakati  na kwa kuzingatia viwango vilivyowekwa na serikali.








KATIKA VIDEO

Post a Comment

0 Comments