SUAMEDIA

Watafiti na Wadau wa kilimo wametakiwa kuimarisha ushirikiano ili kukifanya Kilimo Ikolojia

 

Na.Tatyana Celestine.

Watafiti na Wadau wa kilimo wametakiwa kuimarisha ushirikiano ili kukifanya Kilimo Ikolojia nchini  kuwa na tija  kwa mkulima mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

 Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Utafiti  na Uzamili  kutoka Chuo Kikuu Cha Sokoine Cha Kilimo SUA Prof. Ezron Karimulibo  katika uzinduzi wa Kitovu cha Kilimo Ikolojia awamu ya pili mjini Morogoro ambapo amesema  Kilimo Ikolojia kinaendelea kupewa kipaumbele nchini  kwa sababu  ni kilimo ambacho  kinajali na kutunza mazingira  na kuongeza kuwa ni kilimo kinachoweza  kufaidisha  vizazi na vizazi.

’Katika suala la kilimo ikolojia tunalipa kipaumbele kwa sababu  ni kilimo ambacho kinajali na kutunza mazingira  lakini pia uendelevu wa vizazi na vizazi  vinaweza kunufaika  na kilimo ikolojia  nchini mwetu lakini zaidi ya hapo tumewaasa watafiti  na wadau wa kilimo katika mkutano huu  kuendeleza umoja kwa sababu mazingira  ya ushirikiano inabidi yaboreshwe zaidi  baada ya kipindi hiki cha UVIKO 19 kwasababu wasitazamie sana ufadhili kutoka nje ya nchi  lakini tukiboresha   ushirikiano wetu kwa taasisi za ndani  tunaweza tukafikia malengo makuu katika kukiendeleza kilimo hiki,’’ amesema Prof. Karimulibo .

Aidha Prof. Karimulibo amesema kuanzia kipindi cha mwaka 2019 hadi mwaka 2020 wamewafikia wakulima wa mikoa ya Morogoro, Arusha na Singida lengo likiwa ni kutoa elimu  juu ya ulimaji wa kilimo ikolojia  na jinsi wanavyoweza kupata faida kupitia kilimo hicho.

 

Prof.  Karimulibo  ameongeza kuwa kilimo ikolojia kinaweza kuwa mkombozi kwa wakulima  kutokana na ghala za mbolea za kisasa  kuwa juu  ambapo amesema zaidi ya asilimia 80 ya wakulima kote nchini  wanaishi vijijini na wanategemea kilimo kuendesha maisha yao ya kila siku.

Tunaamini kwamba kuja na teknolojia hii mbadala  ya kilimo ikolojia basi tunaamini tutaweza kuinua  tija na kuinua uzalishaji wa mazao yatokanayo na kilimo,” amesema Mkurugenzi huyo.

Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa Kitovu cha Kilimo Ikolojia Tanzania Prof. Dismas Mwaseba amesema kuwa mradi ulianza mwaka  2019 na awamu ya kwanza imemalizika mwaka 2021 ambapo mradi umelenga katika  kuboresha maisha ya mkulima  na kufanya uhifadhi wa mazingira.

”Tunategemea katika awamu hii ya pili ambayo tunaianza mwaka huu  2022 na kukamilika 2024  tutaongeza eneo la kufanyia utafiti  kwa kuzingatia mahitaji ya wakulima, kwa ujumla wakulima wamepokea vizuri hizi mbinu mbalimbali za kilimo ikolojia tunazowapatia na tunavyoona serikali ikiweza  kutoa msaada basi wakulima wengi watanufaika na kilimo hiki”, amesema Prof. Mwaseba.

Akizungumzia changamoto kubwa katika kufanya kilimo ikolojia Prof.  Mwaseba amesema kuwa sera iliyopo sasa inajikita zaidi kwenye kilimo ambacho kinahitaji matumizi makubwa ya mbolea na viuatilifu  na kuomba kuwepo kwa mabadiliko ya kisera ambayo yatakiwezesha kilimo ikolojia nchini kuwa rahisi kwa wakulima wote wanaotegemea kilimo kuendesha maisha yao.

 

Uzinduzi huo wa kitovu cha kilimo Ikolojia awamu ya pili  umehudhuriwa na wadau mbalimbali wa kilimo nchini pamoja na wakulima ambapo mradi huo unafadhiliwa  wa MARKNIGHT FOUNDATION pamoja na DANIDA Kutoka Nchini Denmark  huku ukiwa unazihusisha taasisi mbalimbali za Serikali ikiwemo TARI, TARIRI pamoja na taasisi binafsi zinazojihushisha na kilimo hapa nchini.

KATIKA VIDEO

Post a Comment

0 Comments