SUAMEDIA

Vyuo Vikuu vya Kilimo nchini bebeni jukumu la mabadiliko ya kilimo nchini - Mhandisi Robert Gabriel

 

Na Gerald Lwomile

Mwanza

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel amevitaka vyuo vikuu vya kilimo, yaani, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo na Chuo Kikuu Cha Mwalimu Julius K. Nyerere cha Kilimo na Teknolojia, kuhakikisha vinabeba jukumu kubwa katika mabadiliko ya kimuundo ya kilimo nchini.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel akizungumza na washiriki wa Kongamano la Miaka 60 Uhuru 

Akifungua Kongamano la siku moja katika maadhimisho ya Miaka 60 ya Uhuru katika Chuo Kikuu cha Mt. Augustine Jijini Mwanza leo tarehe 01 Desemba, 2021 Mhandisi Gabriel amesema ubebaji huo wa jukumu katika kilimo iwe katika maana pana ya kukuza kilimo kupitia mimea vipando, mifugo, uvuvi na mifumo ya uzalishaji wa misitu pamoja na tasnia ya kilimo inayohusiana nayo.

Amesema ni muhimu kwa Vyuo vikuu hivi kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa weledi kwani ni taasisi muhimu katika kuhakikisha kunakuwa na mageuzi ya uchumi wa nchi hasa katika sekta ya kilimo.

Mhandisi Gabriel amesema Mwaka 1961 wakati Tanzania Bara inapata uhuru, mchango wa kilimo katika mapato ya fedha za kigeni ulikuwa ni zaidi ya asilimia 75 na watanzania waliokuwa wanaendesha maisha yao kwa kutegemea kilimo walikuwa zaidi ya asilimia 90 kati ya Watanzania milioni 9.8.

“Mchango wa sekta ya Kilimo katika Pato Ghafi la Taifa GDP ulikuwa zaidi ya asilimia 70, wakati kilimo kilikuwa kinachangia takribani asilimia 81 ya mapato ya mauzo ya nje. Mapato kutokana na mauzo ya mazao ya kilimo yalikuwa Dola za Marekani Milioni 115 mwaka 1961. Kwa sasa, mchango wa kilimo katika pato la Taifa ni wastani wa asilimia 27.2. Ukuaji huo unaonyesha kuwa kilimo bado kinachangia kiasi kikubwa katika uchumi ingawa kiwango cha uchangiaji kimekuwa kikishuka kutokana na kukua kwa sekta nyingine hususan madini, viwanda, ujenzi na huduma” amesema Mhadisi Gabriel

 

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel wa tatu kushoto akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Uzamili, Utafiti, Uhaulishaji wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalam Prof. Esron Karimuribo wa pili kulia katika banda la maonesho

Amesema pamoja na mafanikio haya sekta ya kilimo imeendelea kukumbwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na uzalishaji wa kujikimu na usio na tija miongoni mwa wakulima wodogo hapa nchini.

“Kwa mfano, uzalishaji wa mahindi uko chini ya tani mbili (tani 1.9) kwa hekari moja badala ya tani 8. Uzalishaji usio na tija miongoni mwa wakulima wadogo hutokana na sababu nyingi ikiwemo mapungufu ya huduma za ugani yanayosababishwa na kutofikiwa kwa uwiano wa afisa mmoja kuhudumia kaya 600 (1:600) au kijiji kimoja (1:1)” amesema Mhandisi Gabriel

Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Mkoa amefurahishwa kuona maonesho ya teknolojia na ubunifu katika uzalishaji wa mazao ya kilimo, ufugaji na uvuvi yaliyofanywa na SUA katika Kongamano hilo.

Ambapo ameipongeza SUA kwa maonesho ya teknolojia mbalimbali ambazo wamezibuni na kuahidi kuhakikisha kunakuwa na maonesho makubwa zaidi ambayo yatasaidia wananchi na wakulima mbalimbali katika ukanda wa Ziwa Victoria.

Awali akimkaribisha Mkuu huyo wa Mkoa ili kufungua Kongamano hilo Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda amesema kongamano hilo ni muhimu ili kutoa uelewa wa mambo mbalimbali kwa wakulima ikiwa ni pamoja na namna ya kuzikabili changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya kilimo


Prof.Christopher Kasanga Mkuu wa Idara ya Mikrobiolojia SUA akiwaeleza wanafunzi wa Shule ya Sekondari Ngaza namna wanavyotumia mashine za kisasa kutambua vimelea vya magonjwa kwa njia ya vinasaba 

Prof. Chibunda amesema katika miaka 60 ya Uhuru SUA imefanikiwa kutoa wataalamu mbalimbali wa kilimo ambao wamesaidia kuhakikisha sekta ya kilimo nchini inakua kwa kufanya tafiti na kutoa huduma mbalimbali za ugani hususani kwa wakulima waliko vijijini

Aidha ameongeza kuwa SUA imeendelea kuzalishaji miche ya matunda ikiwemo kwa njia ya chupa, kutoa chanjo za wanyama na uthibiti wa visumbufu vya mazao ya kilimo na wanyama

Naye Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mwalimu Julius K. Nyerere cha Kilimo na Teknolojia Prof Lesakit Mellau akitoa neno la shukrani kwa mgeni rasmi amesema Serikali imekuwa ikiunga mkono juhudi za kilimo nchini ikiwa ni pamoja na kuendelezwa kwa ujenzi katika vyuo vinavyotoa elimu ya kilimo nchini

Kongamano hilo la kuadhimisha miaka 60 ya Uhuru lililofanyika leo Desemba 01, 2021 na kubeba kauli mbiu isemayo ‘Mchango wa Sekta ya Kilimo katika Maendeleo ya Tanzania: Mafanikio na Changamoto Miaka 60 Baada ya Uhuru’. limeshirikisha chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Chuo Kikuu cha Mwalimu Julius K. Nyerere cha Kilimo na Teknolojia, na mwenyeji Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino cha Tanzania (SAUT)


Post a Comment

0 Comments