SUAMEDIA

Shule Ya Udereva yafunguliwa Rasmi, SUA yapongezwa

 Na Farida Mkongwe

Serikali wilayani Morogoro imekipongeza Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA kwa uamuzi wa kuanzisha Shule ya udereva wa mitambo ya kilimo, magari na pikipiki ambao utapunguza matumizi ya nguvu kazi katika uzalishaji na hivyo kusaidia taifa kufikia malengo ya uzalishaji chakula.





Pongezi hizo zimetolewa na Mkuu wa wilaya ya Morogoro Bw. Abert Msando wakati wa ufunguzi wa shule hiyo uliofanyika Novemba 19, 2021 kwenye viwanja vya Kampasi ya Edward Moringe mjini Morogoro.

Bw. Msando amesema pamoja na shule hiyo ya udereva kulenga wanafunzi wa SUA lakini pia itakuwa ni fursa ya kuwafundisha vijana wengine kupata ujuzi wa namna ya kuendesha mitambo mbalimbali ya kilimo na hivyo kuwa njia mojawapo ya kuwafikia wakulima wengi nchini.

Amesema SUA imekuwa Chuo Kikuu cha mfano nchini katika kubuni na kuibua Miradi na Programu mbalimbali zinazolenga kuwajengea vijana uwezo na kuwawezesha kujipatia ajira hususani katika sekta ya kilimo na kilimo biashara  

“Chuo hiki ni cha kwanza kutoa mafunzo ya mitambo ya kilimo na udereva katika nchi yetu yanayoendeshwa na Chuo kikuu, vijana watakaojifunza katika shule hii watapata fursa ya kukutana na wataalam waliobobea katika fani mbalimbali zikiwemo za udongo, mimea, uhandisi kilimo na umwagiliaji na fani nyingine za kilimo cha kisasa......", alisema Bw. Msando.

Awali akimkaribisha mgeni rasmi Makamu Mkuu wa Chuo cha SUA Prof. Raphael Chibunda amesema SUA baada ya kupokea matrekta 10 kutoka kwa Hayati Rais John Magufuli kilijitathmini na kuona sababu za msingi za kuanzisha  shule hiyo kwa ajili ya wanafunzi wa SUA ambao hasa mitaala yao inawataka kujifunza udereva na ufundi wa mitambo hiyo.

“Shule hii itasaidia sana wanafunzi wetu kupata mafunzo, cheti na leseni ya utumiaji wa mitambo ya kilimo (Daraja G) na kuwasaidia kupata ajira au kujiajiri pale wanapohitimu masomo yao na pia itasaidia kuifikia jamii yenye uhitaji wa mafunzo na ujuzi wa kuendesha mitambo ya zana za kilimo hususani vijana”, alisema Prof. Chibunda.

Mafunzo ya Shule hiyo yatakayotolewa kwa awamu nne kwa mwaka yatakuwa ya muda wa wiki tano hadi nane kutegemeana na aina ya kozi na awamu ya kwanza itaanza mwezi Januari na Februari mwakani.


 

 

Post a Comment

0 Comments