SUAMEDIA

Vyuo Vikuu anzisheni program zinazoendana na rasilimali tulizonazo - Dkt Akwilapo

 Na Farida Mkongwe, Dar es Salaam

Vyuo Vikuu nchini vimetakiwa kuanzisha programu za masomo zinazoendana na rasilimali zilizopo pamoja na kuboresha maisha ya watanzania kwa kuongeza tija kwenye sekta ya kilimo, afya, madini, mafuta na gesi.


Mgeni rasmi Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leornad Akwilapo aliyesimama kushoto akibadilishana mawazo na Makamu wa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA katikati mara baada ya kutembelea banda la SUA


Wito huo umetolewa na Katibu Mkuu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leornad Akwilapo wakati akifungua Maonesho ya 15 ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia yanayofanyika katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.

Dkt. Akwilapo amesema iwapo vyuo vikuu nchini vitakuwa na programu za masomo zinazoendana na mahitaji ya watanzania basi hata suala la kupeleka wagonjwa nje ya nchi kwa ajili ya matibabu halitakuwepo na badala yake wagonjwa watatoka nje ya nchi kuja kupata matibabu hapa nchini kama ambavyo inafanyika kwa sasa ambapo baadhi ya vituo vinapokea wagonjwa kutoka nje ya nchi kwa ajili ya matibabu.


Wadau mbalimbali wakisikiliza hotuba ya ufunguzi ya mgeni rasmi hayupo pichani, katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam

"Tusingependa kuwa tunapeleka wagonjwa wetu nje kutibiwa bali nchi za nje ndio zilete wagonjwa wake hapa nchini, tulishaanza hivyo tuzidi kujiimarisha zaidi ili na sisi tuwe kama India ambapo watu wanapeleka wagonjwa wao kila siku", alisema Dkt. Akwilapo.

Katika hatua nyingine Katibu Mkuu huyo amezitaka taasisi zote za vyuo vikuu nchini kutafuta namna ya kupanua udahili wa vyuo hivyo ili kuendana na kasi la ongezeko la udahili lililopo kuanzia ngazi ya shule za msingi ambalo linatokana na uamuzi wa serikali wa kutoa elimu bure kwa shule za msingi

"Ongezeko hili likifikia hatua ya vyuo vikuu ni wazi vyuo vyenu vitaathirika, wito wangu vyuo vyote mjipange kuanzia sasa kuhakikisha muda utakapofika kusiwe na taharuki bali kuwe na nafasi za kutosha wanafunzi kuweza kujifunza", alisisitiza Dkt. Akwilapo.

Akizungumzia upande wa tafiti, Dkt. Akwilapo ametoa wito kwa vyuo vikuu na taasisi zote za utafiti nchini kujielekeza katika kutoa tafiti zenye lengo la kujenga msingi wa uchumi wa viwanda hususani tafiti za teknolojia na bidhaa za viwandani.

Akitoa neno la shukrani  Mwenyekiti wa Kamati ya Makamu Wakuu wa Vyuo Vikuu na Wakuu wa Vyuo Vikuu Vishiriki vya Tanzania Prof. Raphael Chibunda ambaye pia ni  Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA ameiomba Tume ya Vyuo Vikuu nchini TCU kuyapanua maonesho hayo ili vyuo vipate nafasi ya kuonesha shughuli nyingine zinazofanywa na vyuo hivyo zikiwemo tafiti na ushauri.


Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Prof. Raphael Chibunda akitoa neno la Shukrani kwa Mgeni rasmi



Post a Comment

0 Comments