SUAMEDIA

Wakulima watakiwa kujua afya za mashamba yao ili wapate mavuno mazuri

 Na Farida Mkongwe, Dar es Salaam

Wakulima nchini wametakiwa kufuata kanuni na taratibu bora za kilimo ikiwa ni pamoja na kujua afya za mashamba yao kabla ya kuanza kulima ili waweze kupata mavuno yenye tija.


Baadhi ya wananchi waliojitokeza kwa wingi katika banda la SUA wakipata maelezo na kufanya udahili wa kujiunga na chuo hicho kwenye maonesho ya Vyuo Vikuu (TCU) jijini Dar es Salaam


Ushauri huo umetolewa na Mtaalamu wa Maabara ya Udongo kutoka Ndaki ya Kilimo, Idara ya Sayansi ya Udongo na Jiolojia wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Bw. Stevenson  Pelegy Noah wakati akizungumza na SUAMEDIA katika Maonesho ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia yanayofanyika jijini Dar Es Salaam.

Bw. Noah amesema ili kujua afya ya shamba mkulima anatakiwa apime udongo na kujua virutubisho vilivyomo kwenye udongo vinafaa kwa mazao ya aina gani, kujua aina ya mbolea inayohitajika pamoja na kupata ushauri kutoka kwa wataalamu ili aweze kufikia malengo yake.


Makamu wa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Prof. Raphael Chibunda aliyesimama kulia akikagua banda la SUA anayefuata ni Dkt.Nyambilila Amour Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Shahada za Awali SUA


“Hapa tumekuja na maabara ya udongo inayobebeka, kazi yake kubwa ni kupima virutubisho vya mimea vilivyopo kwenye udongo, kwa hiyo mtu akija na sampuli ya udongo kutoka shambani kwake kama katumia vile vigezo tunavyohitaji basi tutampimia na kumpa ushauri bure”, alisema Bw. Noah.

Amesema kwa wakulima ambao watashindwa kupima udongo wanaweza kugundua mapungufu yaliyopo kwenye udongo uliopo kwenye mashamba yao kwa kuangalia rangi na aina ya udongo uliopo shambani kwake na pia anaweza kutumia dalili mbalimbali ambazo zinajitokeza kwenye mimea inayoota mashambani.

Amezitaja baadhi ya dalili hizo kuwa ni mmea kudumaa na kuwa na rangi ya njano, majani ya mwanzo kukauka mapema, mmea kuwa na rangi ya zambarau na mimea kuwa na michirizi ya njano ambapo amesema hizo ni dalili za mimea kuwa na mapungufu ya nitrojeni, fosforas, salfa au potassium ambapo mkulima anatakiwa kupata ushauri kutoka kwa wataalamu ili ajue namna ya kukabiliana na mapungufu hayo.




Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt Leonard Akwilapo wa tatu kutoka kushoto ambaye ndiye mgeni rasmi akisikiliza maelezo kutoka kwa Makamu wa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Prof Raphael Chibunda wa pili kulia



Post a Comment

0 Comments