Na: Farida Mkongwe
Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga,
ametembelea banda la Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) katika Maonesho ya
Nanenane yaliyoanza Agosti 1, 2026, na kujionea teknolojia mbalimbali za kisasa
zinazolenga kuimarisha uzalishaji wa mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi.
Waziri Kapinga alipokelewa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo
anayeshughulikia Mipango, Fedha na Utawala, Prof. Amandus Muhairwa, kwa niaba
ya Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. Raphael Chibunda.
Katika ziara hiyo, Mhe. Kapinga alijionea teknolojia zinazohusu uzalishaji wa mazao, ufugaji wa kisasa, uvuvi na uchakataji wa mazao, pamoja na bidhaa mbalimbali za kibunifu zinazotokana na tafiti zinazofanywa na chuo hicho. Aidha, alipata maelezo kutoka kwa wataalamu na watafiti kuhusu matumizi na manufaa ya teknolojia hizo kwa wazalishaji na jamii kwa ujumla.
Ushiriki wa SUA katika Maonesho ya Nanenane unaendelea kuwa jukwaa muhimu la kuunganisha tafiti, teknolojia na matumizi yake katika mazingira halisi ambapo kupitia maonesho hayo, chuo kinatoa elimu, ushauri wa kitaalamu na teknolojia kwa wakulima, wafugaji, wavuvi na wadau wengine, kwa lengo la kuongeza tija na kuchangia maendeleo endelevu ya sekta ya kilimo nchini.



0 Comments