SUAMEDIA

Elimu Kilimo inaweza kutatua changamoto za usalama wa chakula na mabadiliko ya tabia nchi

 Na: Gerald Lwomile

Serikali imesema elimu ya kilimo ni nguzo muhimu katika kukabiliana na changamoto za usalama wa chakula, mabadiliko ya tabianchi, na ajira kwa vijana.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Bw. Gerald Mweli (kushoto) akikabidhi zawadi 

Akizungumza katika hafla ya Majalisi ya 42 ya ugawaji tuzo kwa wanafunzi na watumishi waliofanya vyema kitaaluma, utafiti na ubunifu katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Bw. Gerald Mweli amesema utaratibu  huo ni ishara ya safari ndefu ya umahiri, ubunifu, na kujituma inayokipambanua chuo hicho.

Amesema chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, serikali imeendelea kuwekeza katika program mbalimbali za kuwajengea vijana uwezo katika kilimo kama BBT, SUA STEPS na Mpango wa Kukuza na Kuendeleza Kilimo Biashara AIP, ambazo zinawawezesha vijana kujiajiri na kuwa wabunifu katika mnyororo wa thamani wa kilimo.


“Elimu, hasa katika fani ya kilimo, lazima ishughulikie mahitaji halisi ya jamii yetu. Kutokana na changamoto zinazojitokeza katika eneo la usalama wa chakula, mabadiliko ya tabianchi, na ukosefu wa ajira vijijini, Taasisi kama Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo zimekuwa muhimu zaidi kuliko hapo awali” amesema Mweli.

Amesema SUA ina wajibu mkubwa si tu kwa Tanzania bali pia kwa bara la Afrika katika kutoa wahitimu na watafiti watakaosaidia katika uzalishaji wa chakula ili kukabiliana na ukosefu wa chakula na kuboresha mifumo ya chakula duniani.



Kwa upande mwingine, Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Bw. Mweli ameipongeza SUA kwa kupitia upya mitaala yake ili iendane na mahitaji ya soko la ajira la karne ya 21.



Akimkaribisha mgeni rasmi katika Majalisi hayo Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda amesema zaidi ya vijana na wanataaluma 180 wamefanya vizuri katika masomo, utafiti na ubunifu mbalimbali na wanapata zawadi kuanzia shilingi elfu 50 hadi milioni moja.

Prof. Chibunda amewapongeza wahitimu wote waliofanya vizuri katika masomo yao na kuwa ana matumaini makubwa wataenda kufanya vizuri kila wanapokwenda na katatua changamoto mbalimbali katika jamii inayowazunguka.

Naye Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalam Prof. Maulid Mwatawala amesema utaratibu huo wa kawaida wa chuo kutoa zawadi kwa wanafunzi na wanataaluma waliofanya vyema katika masomo na tafiti ni kichocheo cha kuongeza ufanisi katika masomo, utafiti na ubunifu.



Post a Comment

0 Comments