SUAMEDIA

Vyombo vya habari simamieni na kutenda haki katika habari za uchaguzi mkuu - Prof. Kabudi

 Na: Farida Mkongwe

Vyombo vya habari nchini vimetakiwa kusimamia na kutenda haki na usawa katika kuhabarisha jamii kuhusu Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 ili wananchi wapate elimu itakayowasaidia  kufanya uchaguzi sahihi wa viongozi watakaowaongoza na kuliongoza Taifa kwa ujumla.

Waziri wa Habari, Utamaduni , Sanaa na Michezo Prof. Palamagamba Kabudi (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na Wakurugenzi na wawakilishi wa Wakurugenzi wa vyombo vya habari nchini.

Kauli hiyo imetolewa Februari 13, 2025 na Waziri wa Habari, Utamaduni , Sanaa na Michezo Prof. Palamagamba Kabudi wakati akifungua Mkutano wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji Nchini unaofanyika jijini Dodoma.

Prof. Kabudi amesema vyombo vya habari vya utangazaji nchini kupitia vipindi mbalimbali vina nafasi kubwa ya kutoa elimu kwa jamii na kuijengea uelewa utakaochangia katika upatikanaji wa viongozi bora watakaoleta maendeleo nchini.

Aidha Prof. Kabudi ametoa wito kwa vyombo vya habari nchini kutoa taarifa za mara kwa mara kuhusu utabiri wa hali ya hewa unaotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ili jamii ichukue tahadhari kuhusu athari za mabadiliko ya tabianchi.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA) Dkt. Jabir Kuwe Bakari amesema mamlaka hiyo ina imani kupitia mshauri wa kitaalam kutoka Uingereza anayefanya kazi na mamlaka hiyo wanatajia kuja na sera nzuri za usimamizi wa vyombo vya habari ikiwa ni pamoja na kupitiwa upya kwa gharama mbalimbali ikiwemo gharama za leseni ambazo mara kadhaa zimelalamikiwa kuwa ni kubwa.

Mkutano huo wa siku mbili wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji Nchini uliobeba  Kauli Mbiu isemayo “Wajibu wa Vyombo vya Utangazaji Kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2025" umeenda sambamba na maadhimisho ya Siku ya Redio Duniani ambayo yamebeba Kauli Mbiu isemayo “Redio na Mabadiliko ya Tabianchi”.

Post a Comment

0 Comments