SUAMEDIA

SUA na Japan kusaini Makubaliano ili kukabiliana na magonjwa yanayotoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu

Na Hadija Zahoro

Watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) na watafiti kutoka Japan wamesaini Mkataba wa Makubaliano ili kujadili namna ya kutekeleza mradi ambao unahusiana na kukabiliana na magonjwa makuu mawili ambayo yanatoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu yanayojulikana kama ugonjwa wa kutupa mimba (Brucellosis)  na Kifua kikuu(Zoonotic Tubeculosis) kwa kutumia dhana ya afya moja 

Mradi huo utakaotekelezwa baina ya watafiti kutoka SUA utashirikiana na watafiti wengine Tanzania kutoka NIMR, MUHAS pamoja na vyuo vingine kutoka Japan ikiwemo Chuo Kikuu cha Rakuno Gakuen na Obihiro ambao utafanyika katika wilaya zote za Mkoa wa Morogoro.

Akizungumza na SUA Media mara baada ya utiaji saini wa makubaliano hayo yaliyofanyika Septemba 19, 2023, Dkt. Coletha Mathew, Mtafiti na Mhadhiri Mwandamizi wa Ndaki ya Tiba ya Mifugo na Afya ya Jamii katika Idara ya Anatomia na Patholojia, ambaye amemwakilisha Mkurugenzi wa Mradi huo Prof. Esron Karimuribo amesema kuwa mradi huo ni muhimu  kwa chuo na taifa kwa ujumla kwani unaenda kukabiliana na magonjwa ambayo yapo katika jamii kwa muda mrefu.

‘‘Sisi kama SUA tutafaidi kwa maana ya kwamba utafiti huo utazalisha machapisho ambayo yatakitangaza chuo chetu lakini pia baadhi ya kazi za chuo mbali na kufanya utafiti na kufundisha lakini pia ni kupeleka huduma za ugani kwa jamii kwa hiyo jamii itapata uelewa wa namna gani kwa pamoja tutakabiliana na magonjwa hayo  kwa kukubaliana kwa pamoja sisi , jamii pamoja na watafiti wa Japan’’ anasema Dkt. Coletha.

‘‘Mbali na faida hizo, lakini pia kutakuwa na kipengele cha kujengea uwezo watafiti wetu wa Tanzania pamoja wanataaluma wetu kwa hiyo SUA pia itafaidika kwa namna hiyo’’ anaongeza Dkt. Coletha.

Kwa upande wake Mshauri Mkuu wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA),Dkt. Yumi Kirino ameeleza kuwa ndani ya miaka hiyo mitano ya utekelezaji wa mradi, wamechagua kwenda kuyafanyia kazi magonjwa hayo mawili ambayo yanaambukizwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu kwa sababu bajeti ya kuzuia aina hiyo ya magonjwa  haijitoshelezi  katika nchi nyingi.

Nae Katibu Tawala Msaidizi sehemu ya Uchumi na Sekta za Uzalishaji Ofisi ya Mkoa wa Morogoro, Dkt. Rozalia Rwegasira, ameeleza kuwa  Mkoa ni wanufaika wa mradi huo kwani utakwenda  kuwasaidia wananchi wa Mkoa wa Morogoro kutambua magonjwa hayo na namna ya kujikinga.

Ameeleza kuwa kutokana na uwepo wa mifugo mingi hivyo kuna matumizi ya mazao ya mifugo ikiwemo nyama pamoja na maziwa, hivyo mradi huo utakwenda kuacha alama katika mkoani kwani  unakwenda kupunguza athari za magonjwa hayo  yanayotoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu. 

Mradi huo unaofadhiliwa na JICA na AMED, utaanza  mwezi Julai 2024 na utatekelezwa ndani ya miaka mitano. 




KATIKA VIDEO

Post a Comment

0 Comments