SUAMEDIA

Waliomaliza kidato cha sita watakiwa kufika banda la SUA kujisajili moja kwa moja

 

Na Farida Mkongwe

Wazazi na wanafunzi waliomaliza kidato cha sita ambao wanatarajia kujiunga na Vyuo Vikuu kwa mwaka wa masomo 2023/2024 wametakiwa kufika kwenye Banda la Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) lililopo   katika viwanja vya Maonesho ya Vyuo Vikuu kwenye viwanja vya Mnazi mmoja jijini Dar Es Salaam ili waweze kusajiliwa na Chuo hicho.

Afisa Udahili wa SUA Bi. Grace Kihombo (kulia) akitoa maelezo kwa mwanafunzi anayefanya usajili katika Chuo hicho

Wito huo umetolewa na Afisa Udahili wa Chuo hicho Bi. Grace Kihombo Julai 17, 2023 wakati akizungumza na SUAMEDIA katika viwanja hivyo ambapo amesema mwanafunzi akifika katika banda hilo atapewa elimu kuhusu kozi mbalimbali zinazotolewa na SUA na baada ya hapo kama atakuwa tayari atasajiliwa moja kwa moja.

“SUA tumekuja na vipeperushi ambavyo mtu akija hapa anasoma na atachagua kozi ambayo anaipenda kwa hiyo tunawakaribisha wote ambao wapo karibu na viwanja vya mnazi mmoja waje tunasajili live kabisa na baada ya hapo mwanafunzi atakuwa anasubiri kuchaguliwa”, amesema Bi. Grace.

“Kwa hiyo tunawahamasisha wazazi wote wenye watoto wao ambao wamemaliza kidato cha sita lakini na wanafunzi waliopo tunawahimiza waje hapa kwenye hivi viwanja vya Mnazi Mmoja ili waje wafanye maombi maana hapa kuna usaidizi wa kutosha”, amesisitiza Afisa Udahili huyo kutoka SUA.

Aidha amewataka wazazi na wanafunzi wanaotarajia kujiunga na vyuo mbalimbali kuelewa kuwa pamoja na kozi za kilimo, SUA pia kuna kozi za Uchumi na Biashara, Sanaa, Misitu, Wanyamapori na Utalii na nyinginezo ikiwemo kozi za ualimu ambapo Chuo kinatoa walimu wazuri wa kozi za Sayansi.

Maonesho ya 18 ya Vyuo Vikuu ambayo yameandaliwa na Tume ya Vyuo vikuu Tanzania kwa mwaka huu 2023 yamebeba kauli mbiu isemayo “Kukuza Ujuzi Nchini Kupitia Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia kwa Uchumi Imara na Shindani”.




Post a Comment

0 Comments