SUAMEDIA

SUA na Teknolojia ya Umwagiliaji kwa njia ya Simu pamoja na Ndege bila rubani shambani

 

Winfrida Nicolaus

Kupitia Maonesho ya 29 ya Wakulima, Wafugaji na Wavuvi Kanda ya Mashariki, Shule Kuu ya Uhandisi na Teknolojia SUA imeandaa na kuonesha Teknolojia ya kisasa ya Umwagiliaji kwa njia ya simu pamoja na Ndege bila rubani shambani.





Amebainisha hayo Mteknolojia kutoka Shule Kuu ya Uhandisi na Teknolojia iliyopo Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Paul Reuben wakati akizungumza na SUAMEDIA kwenye Maonesho hayo kuhusiana na Teknolojia ya Mafunzo ya Zana za Kilimo pamoia na Mafunzo ya Udereva wa Mitambo ya Kilimo, Magari na Pikipiki.

Amesema Teknolojia ya Simu inamuwezesha Mkulima ambaye ameshindwa kufika shambani kutokana na shughuli nyingi za hapa na pale kumwagilia bila yeye kuwepo shambani kwa kutuma meseji ya neno mwagilia na mfumo unajifungua na kuanza kumwagilia na akihitaji kuufunga anatuma neno funga au zima na unajifunga wenyewe moja kwa moja.

Bw. Reuben amesema Teknolojia hiyo ya Umwagiliaji kwa njia ya simu itamjulisha mkulima pia endapo maji ya kumwagilia yameisha ambapo utamsaidia kuweza kutafuta namna ya kuweka maji na shughuli ya umwagiliaji kuendelea katika shamba lake.

Amesema Teknolojia nyingine ni matumzi ya Ndege bila Rubani Shambani ambayo inauwezo wa kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa ambapo inaweza kumtaarifu Mkulima kama mbolea imepungua kwenye zao lake na kumfanya ajue kiasi gani cha mbolea kinahitajika kulingana na upungufu na kuweza kuweka mbolea mahali sahihi.

“Mkulima anacho kifanya akiwa eneo lolote hata nje ya nchi anaweza akaamuru mfumo ufanye anachokihitaji kifanyike shambani na kitafanyika iwe kumwagilia au kumjulisha changamoto zilizopo shambani mfano maji yameisha”, amesema Bw. Reuben

Aidha amesema hapo baadaye wataanza kutumia Sensa ambazo zitawekwa shambani na zinauwezo wa kusema kiasi cha unyevunyevu ulioko kwenye shamba ambapo mfumo una uwezo wa kujiseti wenyewe na kutoa taarifa.

Naye Fundi Sanifu wa Zana za Kilimo katika Shule Kuu ya Uhandisi na Teknolojia SUA Bakari Mohamed amesema katika Maonesho hayo wanatambulisha pia Shule ya Udereva wa Magari, Pikipiki pamoja na Uendeshaji wa Mitambo ya Kilimo kama vile Matrekta, Makatapila, Mitambo ya kuvunia mahindi na mengineyo.

Amesema kuna faida kubwa endapo mtu atajifunza Udereva kutoka SUA kwasababu wanatoa elimu kwa Vitendo kutokana na kuwa na vifaa vyote ikiwemo mitambo yenyewe na elimu inatolewa kwa bei nafuu na mwanafunzi atajifunza kwa muda mfupi pia mwanafunzi hawezi kumaliza mafunzo bila kufanyiwa majaribio na Askari wa Usalama barabarani ambapo itampelekea leseni yake kuwa bora zaidi.

 

 

 

 

 

 

Post a Comment

0 Comments