SUAMEDIA

Maabara inayotembea SUA imechangia kudhibiti magonjwa ya mlipuko

 NA: Farida Mkongwe

Maabara inayotembea iliyopo Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA kwa kiasi kikubwa imechangia kudhibiti magonjwa ya mlipuko kutokana na Maabara hiyo kuwa na uwezo wa kuyafikia maeneo yenye ugonjwa kwa haraka.

Hayo yamebainishwa na Dkt. Edson Kinimi ambaye ni Mhadhiri, Idara ya Fiziolojia, Biochemia na Famakolojia iliyopo Ndaki ya Tiba ya Wanyama na Sayansi za Afya SUA wakati akizungumza na SUAMEDIA katika viwanja vya Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki yanayofanyika mkoani Morogoro.

Dkt. Kinimi amesema tangu kuanza kutumika kwa Maabara hiyo kumekuwa na unafuu kwa Serikali na Wananchi kwa ujumla kwa sababu kumekuwa na uwezo wa kuyadhibiti kwa haraka magonjwa ya milipuko.

“Hili gari lina uwezo wa kwenda sehemu korofi ambazo hazifikiki kiurahisi hata nyakati za mvua, gari hili lina uwezo wa kufika sehemu hizo na kwa sababu lina vifaa vinavyosaidia kujua vinasaba vyenye magonjwa yanayosababishwa na Virusi, Bakteria au magonjwa ya Kuvu basi vipimo vinafanywa na majibu kupatikana hapo hapo”, amesema Mhadhiri huyo.

Akizungumzia chimbuko la Ubunifu wa Maabara hiyo inayotembea, Dkt. Kinimi amesema dhana hiyo imekuja baada ya kuwepo kwa magonjwa ya milipuko na kuwepo ugumu wa kuyafikia maeneo husika.

“Ubunifu wa hii Maabara inayotembea umetokana na kutaka kufika maeneo husika ambayo yanakuwa na maambukizi hivyo tukafikiria namna ya kufika maeneo husika ili tuweze kufanya uchunguzi na kutoa majibu kwa haraka’, amefafanua Dkt. Kinimi.

Ameongeza kuwa wakati wa ugonjwa wa Korona waliweza kufanya kazi na Wizara ya Afya na Taasisi ya Taifa ya Utafiti na kusaidia kwa mara ya kwanza kubaini vinasaba vya ugonjwa wa Korona.

“Na juzi juzi tu ulisikia habari ya homa ya Mgunda chuo cha SUA kimeweza kuhusika kupima kupitia Taasisi yake ya SACIDS”, amesema Dkt.Kinimi.

 




 

 

Post a Comment

0 Comments