NA:Farida Mkongwe
Imeelezwa kuwa Mfumo wa
Afya Data ambao umebuniwa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA kuwa ni
mfumo ambao unasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza madhara yatokanayo na
magonjwa ya Mlipuko.
Hayo yameelezwa na Dr.
Robert Andrew Maduka ambaye ni Mratibu Msaidizi wa Mradi unaojishughulisha na
Tafiti za Magonjwa Ambukizi ya Binadamu na Wanyama SACIDS wakati akizungumza na
SUAMEDIA kwenye viwanja vya Maonesho ya 29 ya Nanenane Kanda ya Mashariki
yanayofanyika Mkoani Morogoro.
Dr. Maduka amesema mfumo
huo wa Afya Data unatumika kutoa taarifa za dalili za magonjwa ya mlipuko
ambapo watu waliopo kwenye maeneo yenye dalili za magonjwa hayo wanawasiliana
na watoa huduma za afya kwa kutuma ujumbe wa dalili wanazoziona na baadae watoa
huduma za afya wanafuatilia na kubaini tatizo
“Mfumo huu unaweza
ukaupakua na ukawa nao kwenye Simu yako ya mkononi, ukishakuwa nao basi ni
rahisi kuripoti taarifa za dalili za magonjwa ya milipuko iwe kwa binadamu au
wanyama kwa maana ya mifugo”, amesema Dr. Maduka.
Akizungumzia faida za
mfumo huo Mratibu huyo amesema licha ya
kusaidia kufikisha taarifa za magonjwaya mlipuko kwa haraka lakini pia
unasaidia watu wengi kushiriki kutoa taarifa kwa sababu kabla ya mfumo huo kuna
watu walikuwa hawajui pahali sahihi pa kufikisha taarifa licha ya kujua
matatizo yaliyopo kwenye jamii zao.
Amesema kwa sasa mfumo huo bado upo kwenye uangalizi na kazi katika wilaya mbalimbali zikiwemo Kilosa, Malinyi, Mvomero, Gairo, Ulanga na Ngorongoro ambapo tayari mafunzo yameshatolewa kwa watoa huduma za afya ngazi ya jamii ya namna ya kutumia mfumo huo na kuzifanyia kazi taarifa zinazotolewa.

0 Comments